Na George
Marato,Musoma
MBUNGE wa
Musoma vijijini Nimrod Mkono,ameishutumu Serikali kwa kushindwa kudhibiti
vitendo vya mauaji ya kinyama na kikatili wanafanyiwa wanawake katika baadhi ya vijiji
vya tarafa ya Nyanja jimboni humo huku akisema Serikali imekuwa ikitumia nguvu
kubwa kulinda wanyama pori kuliko binadamu.
Mkono ambaye
kitalum ni mwanasheria,alitoa kauli hiyo juzi katika kijiji cha Mugango katika halmashauri
ya Musoma wilayani Butiama baada ya watu wasijulikana kumnyonga hadi kufa kwa
kutumia kanga yake mwanamke mmoja mkazi hicho Anastazia Mang’ombe (42) kabla ya
kumbaka wakati akiwa shambani kwake.
Mauaji ya
mwanamke huyo ni mwendelezo wa mauaji ya kinyama na kikatili yanayotokea katika
vijiji vya mwambao wa ziwa Victoria vya Nyakatende,Etaro,Nyegina,Mkirira katika
tarafa hiyo yakihusisha wanawake yakiwa ni ya pili kutokea katika kipindi cha wiki
mbili tu baada ya mwanamke mwingine mkazi wa kijiji Kamguruki kata ya
Nyakatende wilayani humo kuuawa pia kwa kunyongwa.
Alisema
tangu kuibuka kwa wimbi la mauaji hayo ya kinyama ambayo hadi sasa yanahusishwa
na imani ya kishirikina hakuna hatua zozote ambazo zimechukuliwa na Serikali licha
ya viongozi wake kutoa kauli za kisiasa ambazo zimeshindwa kumaliza mauaji hayo
na hivyo kuongeza hofu kubwa kwa jamii hasa wanawake.
“Jamani
mauaji haya ya wanawake mwisho wake utakuwa lini,hivi Serikali iko wapi,mbona tembo
mmoja tu akiuawa tunasikia filimbi na ndege zinaruka huku na huku kuwasaka
wauaji iweje leo binadamu hasa hawa wanawake wanauawa bila hatia hatujasikia
serikali wala haijachukua hatua?
“Wakina mama
zangu wanauawa,wanachinjwa kama kuku sijaiona Serikali ikichukua hatua,sasa ni
wakati wa Waziri mkuu na Rais wetu waje hapo ili kutusaidia kukomesha mauaji
hayo ya kikatili…hivi niwaweke wapi wakinama hao sasa wanaishi kwa hofu kubwa”alisema
Mkono kwa uchungu huku akibubujikwa machozi.
Kwa sababu
hiyo mbunge huyo alisema serikali inaonekana kuwapuuza wananchi hao wanauawa kinyama
kwani ina vyombo vya kuwabaini wauaji wote na kuchukuliwa hatua za kisheria.
“Nakwenda bungeni
kupigania hili kwani ni janga la kitaifa ikiwezikana serikali itangaze oparesheni
maalum kama ilivyofanya katika kupambana na ujangili ndani ya hifadhi zetu,hatuwezi
kuacha mama zetu wanauawa kiasi hiki cha kutisha,kwa kweli sitakubali tena wala
kukaa kimya kwa jambo hili”alisema.
Kwa upande
wake mwenyekiti mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ambaye pia ni mkuu wa
wilaya ya Butiama Angelina Mabula,pamoja
na kulaani vikali mauaji hayo amewaka wananchi kutoa ushirikiano kwa jeshi la
polisi ili kuhakikisha wauaji hao wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya
sheria.
“Kwa kweli
hali ni mbaya kweli,nawaomba muwe watulivu kwani matukio haya
yametuchanganya,wiki iliyopita wanawake wawili wameuawa hivi hivi,ukiangalia
matukio yote yanafanana na yanafanyika wazi sasa lazima tujiulize wote hapa
kuna nini?
“Hata
tufanyeje polisi hawawezi tosha kulinda wote lazima tuweka mikakati ya pamoja
katika kushughulikia mauaji haya,kwa muda mfupi tu kwa eneo hili la kata nne wanawake
wanane wameuawa kikatili na mauaji yote yanafanana”alisema DC Angelina.
Kwa sababu hiyo
aliwaomba wananchi kutoa taarifa za kina kwa vyombo vya dola zikiwemo ofisi za
viongozi katika kuhakikisha mauaji hayo yanakomeshwa.
Hata hivyo
mkuu huyo wa wilaya alitoa agizo kwa wanaume kuwasindikiza wake zao mashambani
na katika shughuli nyingene za kutafuta kipato wakati vyombo vya dola
vikipambana na vitendo hivyo vya mauaji hayo.
Alisema
viongozi wa Serikali sasa wameshindwa kuhamasisha shughuli za maendeleo kwani
muda wote wamekuwa wakishughulikia matukio ya mauaji kila kukicha.
Kwa mujibu
mujibu wa mkuu huyo wa wilaya hadi sasa watu watano wamefikishwa mahakamani kwa
tuhuma za mauaji kama hayo huku wanne wakishikiliwa polisi kwa uchunguzi.
Naye katibu
wa CCM wilaya ya Butiama Mercy Mollol,aliomba Serikali kutangaza eneo hilo kuwa
kanda maalum ya kipolisi ili kuongeza idadi ya askari kwaajili ya kukabiliana
na mauaji hayo.
“Kama chama
tumesikitishwa sana na mauaji haya yanayoendelea katika eneo hili,sasa
tunaitaka Serikali chini ya Mh Jakaya Kikwete na IGP Mango kutangaza oparesheni
ya watu wanaua wanawake kabla hatujatangaza maandamano makubwa ya kupinga
ukatili huu”alisema kiongozi huyo wa CCM.
Kamanda wa
polisi mkoa wa Mara,kamishina msaidizi mwandamizi Ferdinand Mtui,akizungumza na
gazeti hili kwa njia ya simu amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba
hadi sasa watu watatu wanashikiliwa kwa mahojiano.
No comments:
Post a Comment