Sunday, April 14, 2013

PAMBANO LA SIMBA NA AZAM TAIFA HOMA YAZIDI KUPANDA NA MAJIGAMBO KILA KONA YA DAR ES SALAAM,

azam vs simba
Na Baraka Mpenja wa Fullshangwe Dar es salaam

Sekunde, dakika, saa zazidi kukatika kuelekea mpambano mkali wa ligi kuu soka Tanzania bara baina ya mabingwa watetezi wa ligi hiyo wekundu wa msimbazi Simba dhidi ya mabingwa mara mbili wa kombe la mapinduzi na wawakilishi pekee wa Tanzania katika michuano ya kimataifa, Azam fc kwenye uwanja wa kisasa wa taifa jijini Dar es salaam.

Azam fc na Simba kwasasa zina upinzani mkubwa sana na kila zinapokutana hakika kipute kinakuwa kikali zaidi ya kawaida.

Simba wanaingiwa uwanjani wakiwa tayari wameshapoteza ubingwa na sasa wanahitaji hata nafasi ya pili ili kupata nafasi ya kucheza mashindano ya kimataifa mwakani wakati lambalamba wao wapo nafasi ya pili na pointi 46 wakihitaji kushinda ili kwasogelea vinara wa ligi hiyo Dar Young Africans.

Kikosi cha Azam kinaonekana kuwa imara zaidi msimu huu kutokana na matokeo wanayopata katika mechi za ligi kuu na michuano ya kombe la shirikisho, wakati Mnyama pori anahaha kweli kutengeneza kikosi kipya baada ya wachezaji wengi `Mafaza` kutemwa na kocha wake Patrick Liewig kwa makosa ya utovu wa nidhamu.

Mechi tatu zilizopita Simba ilicheza bila wakongwe wake, Mwinyi Kazimoto Mwitula, Amir Maftah, Ramadhan Chombo `Redondo`, Haruna Moshi Shaban `Boban`, Ferlix Mumba Sunzu, Komanbil Keita, Juma Said Nyoso na Abdallah Juma baada ya kocha Liewig kuwapiga chini.

Wachezaji Juma Kaseja, Mrisho Khalfan Ngasa `Anko`, Amri Athman Kiemba, Shomary Kapombe Jr, Masoud Nassor Cholo, walibakishwa kwenye kikosi hicho na kucheza michezo yote mitatu dhidi ya Coastal union, Kagera Sugar na Toto Africa.

Kwa sasa Kazimoto na Sunzu wamerejeshwa katika kikosi cha Simba na wanaweza kucheza katika mchezo wa leo endapo mwalimu utapiga hesabu zake vizuri.

Kwa upande wa Azam fc , wao wako kamili kado baada ya nyota wake Said Morad, Erasto Nyoni, Aggrey Morris, Deogratius Munish `Dida` kurejeshwa kikosini baada ya TAKUKURU kushindwa kuwakuta na hatia ya kula mlungula kama walivyoshitakiwa na klabu yao.

Mbali na nyota hao kuwepo, klabu hiyo ina wachezaji hatari katika kufumania nyavu, John Rafael Bocco, Brian Umony, Hamphrey Mieno na Kipre Herman Tchetche.

Lakini wapo wengine machachari kama Abubakar Salum `Sure Boy`, Michael Bolou, Himid Mao, David Mwantika, Khamis Mcha `Vialli` na wengineo.

Hakika mpambano huu ni mkali sana na timu zote zitahitaji ushindi ili kujiweka katika nafasi nzuri ya msimamo wa ligi kuu soka Tanzaniania bara inayoelekea ukingoni.

CHELSEA V MAN CITY WEMBLEY HOMA YAPANDA KWA KASI KUBWA!!

Carlos Tevez na David Luiz
Carlos Tevez na David Luiz
Na Supersport.com

Mabingwa watetezi wa kombe la FA nchini England watakuwa kibaruani leo hii majira ya saa 12 jioni katika uwanja wa taifa wa Wembley kupepetana na mabingwa watetezi wa taji la ligi kuu soka nchini England, klabu ya Manchester city mchezo wa nusu fainali ya pili ya FA.

Miamba hiyo imeshindwa kupambana na mashetani wekundu kuwania taji la ligi kuu msimu huu ingawa Chelsea wamefika hatua ya nusu fainali ya ligi ya UROPA, lakini mchezo huu utakuwa muhimu kwao wote ili kumaliza msimu angalau na kikombe kimoja.

Mshindi wa mchezo wa leo utakumbana naWigan Athletic katika mtanange wa fainali baada ya klabu hiyo  kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya timu ya daraja la Championship, Millwall na kutinga hatua ya fainali.

Kocha wa muda wa Chelsea Rafael Benitez na wa City  Roberto Mancini wote kwa pamoja wanawania kutwaa kombe kwa mara ya pili wakifanya kazi nchini Uingereza.

Mwishoni mwa mwezi februari mwaka huu timu hizo zilikutana katika dimba la Etihad katika mchezo wa ligi kuu na kushuhudia City wakiwabamiza wapinzani wao mabao 2-0,  lakini Benetez amesema amejifunza kwa kiasi kikubwa.

“Tunajua itakuwa mechi ngumu, lakini ni nusu fainali yenye ushindani mkubwa”. Alisema Mhispania huyo aliyetwaa ubingwa wa kombe hilo mwaka 2006 akiwa na wekundu wa Anfield, klabu ya Liverpool.

Benetez aliongeza kuwa City ni timu nzuri, ina kikosi bora na kocha mzuri mwenye uzoefu mkubwa,  lakini watajituma zaidi endapo wanataka kuibuka kidedea katika kipute hicho.
City wanaingia uwanjani wakiwa na kumbukumbu nzuri ya kuwafumua watani zao wa jadi Manchester United mabao 2-1 katika uwanja wa Old Traford jumatatu ya wiki hii mchezo wa ligi kuu soka Uingereza.

Mancini amekuwa na presha kubwa baada ya kuweka rehani ubingwa wake mbele ya united, lakini bado ana nafasi ya kujikusanyia kombe la tatu ndani ya miaka mitatu.
Kocha huyo aliondoa ukame wa City kutotwaa ubingwa wa kombe la FA kwa miaka 35 baada ya kuiongoza klabu yake kunyakua ubingwa mwaka 2011 akiwafunga Stoke city mchezo wa fainali.

Mancini alisema, “nadhani kucheza Wembley ni bonge la mechi kwa mashabiki wote wa soka hivyo ni nafasi muhimu kushuhudia mechi hiyo ya nusu fainali”.

Kocha huyo aliongeza kuwa kila kombe ni muhimu kwa timu zote, lakini kwa upande wao ni muhimu zaidi kwani wana nafasi ya kutinga fainali na kubeba kombe hilo kwa mara ya pili ndani ya miaka mitatu.


SHEHATA AULA MUNICH 1860, SASA MSHAURI WA BENCHI LA UFUNDI!!

Hassan Shehata @action video

Na mtandao

Kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Misri “Mafarao” Hassan Shehata ameteuliwa kuwa mshauri wa benchi la ufundi la klabu ya Munich 1860 inayoshiriki ligi daraja la pili nchini humo
Klabu hiyo imempata Shehata shavu la kuwa mshauri mkuu wa timu zote klabuni hapo yaani timu ya kwanza, ya pili na kikosi cha vijana.

Kocha huyo alisafiri kwenda ujerumani ijumaa ya wiki hii na alianza kazi kwa kuangalia mchezo wa klabu hiyo na kuandika ripoti yake anayotaraji kuiwasilisha kwa viongozi wake.

“Niko hapa kuisaidia timu irejee Bundesliga, Munich 1860 ni timu kubwa sana na nitafanya kila linalowezekana kurudisha heshima ya klabu hii”. Shehata ameuambia mtandao wa Supersport.com

Kocha huyo ameongeza kuwa “nitawasoma wachezaji wote na nitahudhuria mechi zote za klabu hii na baada ya hapo nitakaa chini kupanga mipango thabiti ya kuisaidia timu yangu”.
Munich 1860 inayojulikana kwa jina la TSV Munchen iliundwa miaka 152 iliyopita na makao makuu yake ni jijini Munich Ujerumani.

Timu hiyo inacheza ligi ya daraja la pili ya Bundesliga tangu msimu wa mwaka 2003-2004.

No comments:

Post a Comment