Thursday, February 14, 2013

KATA, TARAFA, JIMBO BORA KWA USALAMA 2012 ZAPEWA TUZO

 

IGP-SAID-MWEMA
 
 
Na. Christina Mponji-Jeshi la Polisi, Dodoma.
………………………………………………………
Wito umetolewa kwa Majimbo, Tarafa na Kata zote nchini kuimarisha dhana ya Polisi jamii na ulinzi shirikishi katika maeneo yao, ili kukabiliana na vitendo vya uhalifu kuanzia ngazi ya familia ambako ndiko hasa chimbiko la uhalifu.
 
Hayo yamesemwa jana na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IJP Said Mwema, wakati akitoa tunuku ya hati ya utendaji bora kwa Kata/Shehia, Tarafa, na Jimbo  zilizofanya vizuri katika mapambano dhidi ya uhalifu nchini kwa mwaka 2012.
 
Tuzo hizo zimetolewa  katika Mkutano Mkuu wa Maofisa wakuu Waandamizi wa Jeshi la Polisi unaoendelea mjini Dodoma katika ukumbi wa Pius Msekwa, ikiwa ni sehemu ya  utekelezaji wa mpango wa maboresho ndani ya jeshi hilo.
 
Kata zilizofanya vizuri ni pamoja na kata ya Bukwe Mkoa wa kipolisi  Tarime Rorya, Kizwite ya mkoani Rukwa, Isansa ya mkoani Mbeya, pamoja na shehia ya Ng’omeni kutoka mkoa wa Kaskazini Pemba.
 
Tarafa zilizofanya  vizuri ni tarafa ya Girango ya mkoa wa kipolisi Tarime Rorya, Lwiche ya mkoani Rukwa, Igamba ya mkoani Mbeya pamoja na Jimbo la Mji Mkongwe la Mkoa wa Mjini Magharibi visiwani Zanzibar ambapo tuzo hizo zimepokelewa na makamanda wa mikoa hiyo  kwa niaba ya kata/shehia na tarafa/majimbo yao.
 
IJP Mwema amesema, endapo kata na tarafa zote nchini zitaimarisha dhana ya ulinzi shirikishi na polisi jamii, ni wazi kuwa matukio ya uhalifu yatapungua kwa kiasi kikubwa na hatimaye kuwa historia.
 
Akiongea katika hafla hiyo Mkuu wa Huduma za Polisi Jamii, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Lazaro Mambosasa alisema kuwa kata na tarafa zilizofanya vizuri, zilikuwa na kiwango kikubwa cha  matukio ya kihalifu lakini kupitia dhana ya ulinzi shirikishi na polisi jamii wamefanikiwa kudhibiti vitendo hivyo huku akitolea mfano kata ya Bukwe ambako kulikuwa na migogoro ya kikabila, na hivi sasa migogoro hiyo imekoma kabisa.  
 
Akiongea kwa niaba ya wenzake, kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya  kamishna Msaidizi Diwani Athumani, amesema jamii sasa imeanza kuelewa umuhimu wa kushirikiana na jeshi la polisi katika mapambano dhidi ya uhalifu na kwamba wamekuwa mstari wa mbele katika kuhamasishana juu ya uanzishwaji wa vikundi vya ulinzi shirikishi.
 
Jeshi la polisi limekuwa likifanya jitihada mbalimbali za kuimarisha hali ya ulinzi na usalama kuanzia ngazi ya kata/shehia, ambapo hivi karibuni wametoa pikipiki kwa wakaguzi tarafa ili kuwarahisishia utendaji katika tarafa zao.

No comments:

Post a Comment