Mratibu wa mpango wa Taasisi isiyo
ya kiserikali ya Wash United Ndugu Femin Mabachi akiwaelezea waandishi
wa habari jinsi watakavyofanya kazi na Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) baada ya kusaini makubaliano ya msingi katika
kushirikiana kutunza mazingira na usafi. Mpango ambao umelenga zaidi
katika kuendeleza mpira wa miguu kupitia mpango wa TFF wa kuendeleza
soka kwa vijana. Mpango huu wa Wash United unafadhiliwa na Serikali ya
Ujerumani kupitia shirika lake la maendelea (GIZ). Kushoto kwake ni
Mshauri wa mambo ya vyanzo vya maji na maendeleo ya mazingira wa GIZ
Ndugu Falk Negrazus na kulia kwake ni Katibu mkuu wa TFF Angetile Osiah.
Makubaliano hayo yalifanyika katika ukumbi wa habari wa TFF uliopo
katika ofisi zake Karume.
……………………………………………………………….
Zaidi ya watu bilioni 2.6
duniani wanaishi bila ya kuwa na vyoo. Barani Afrika, magonjwa ya kuhara
yanayosabishwa na ukosefu wa vyoo na usafi ni hatari zaidi na ndio
yanayosababisha vifo kwa watoto wenye umri chini ya miaka
mitano, hii ni zaidi ya magonjwa kama Ukimwi, Malaria na surua
ikifuatia.
Takwimu kutoka mashirika ya UNICEF na WHO zinaonyesha kuwa
nchini Tanzania zaidi ya asilimia 90 ya watanzania wanaishi katika
mazingira machafu, na asilimia 12 hawana vyoo wala maji. Matokeo yake
zaidi ya watoto 24,000 nchini Tanzania hufariki dunia kila mwaka. Tabia
ya kunawa mikono kwa kutumia sabuni ni njia rahisi na haina gharama
kubwa katika kuzuia magonjwa ya kuhara ambayo haitumiki sana hapa nchini
hasa kwa watoto.
Tatizo kubwa ni kwamba usafi wa mazingira na afya
haupewi kipaumbele katika mawazo ya watu wengi katika vyombo vya habari
na jamii kwa ujumla.
Taasisi isiyo ya kiserikali ya
Wash United inafanya kazi kuweka sawa mambo ya mazingira na usafi katika
ngazi zote mahala popote na kuhamasisha watu kunawa mikono kwa sabuni
kila mara. Wash United ni mpango mpya wa kwanza kutumia nguvu ya mpira
wa miguu na mastaa wake katika kuhamasisha unywaji wa maji safi,
mazingira safi na usafi kwa wote barani Afrika na duniani kote. Katika
kukamilisha mpango wake huu Wash United imeungana na wadau mbalimbali
duniani, kwa hapa Tanzania shughuli zinaendeshwa kwa msaada wa shirika
la maendeleo la Ujerumani (GIZ).
Kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania(TFF)
Shirikisho la mpira wa miguu
Tanzania limekubali kushirikiana na mpango wa Wash United katika
kuhamasusha tabia ya kutunza mazingira na usafi kwenye timu za vijana
kupitia mradi timu za vijana wa shirikisho hilo.
Katibu mkuu wa TFF
Ndugu Angetile Osiah, leo amesaini mkataba wa makubaliano kati ya TFF na
Wash United. “Ushirikiano kati ya Taasisi ya Wash United na Shirikisho
la mpira wa Miguu ni mpya na wa kujitolea katika sekta ya mpira wa miguu
Tanzania. Akiongea kuhusu Wash United, mratibu wa Wash United nchini
Tanzania Ndugu Femin Mabachi alisema “Kupitia mpira wa miguu na kwa
kushirikiana na TFF, tunaweza kutunza mazingira na usafi ‘salama’ na
kuongeza uwiano katika kushughulikia mambo haya katika jamii yetu.
Taifa Stars Kuongoza mpango wa Wash United
Kwa kuungana na Wash United,
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) litakuwa limejiunga na zaidi
ya mastaa 100 wa mpira wa miguu kama Didier Drogba, Michael Ballack,
Arjen Robben, Bayern Munich, Taasisi za Real Madrid na ile ya Barcelona
na pia zaidi ya wananchama 30,000 wa Wash United duniani kote. Nahodha
wa Taifa Stars Juma Kaseja atawaongoza wachezaji wenzake kuwa washiriki
kwenye mpango huu wa Wash United na kushiriki katika kampeni nchini
Tanzania na duniani kote. Zaidi ya yote wachezaji wa timu ya Taifa
watashiriki katika shughuli za mchezo wa mpira wa miguu mashuleni
zitakazofanyika hapa nchini zitazokuwa zikiendeshwa na taasisi hizi.
No comments:
Post a Comment