Sunday, October 7, 2012

WANAFUNZI WALIOTELEKEZWA BAADA YA WALIMU KUKIMBILIA MACHIMBONI WAJISALIMISHA CHADEMA

Geita

KATIKA hali ya kustaajabisha,baadhi ya wanafunzi wanaosoma katika shule ya msingi Ntono iliyopo katika kijiji cha Ntono Kata ya Kamena Wilayani Geita mwishoni mwa wiki iliyopita waliandamana hadi kwa viongozi wa chama cha demokrasia na maendeleo(CHADEMA) ili kufikisha kilio chao cha kutofundishwa kutokana na baadhi ya walimu wa shule hiyo kukimbilia machimboni.

Tukio hilo ambalo liliacha maswali mengi miongoni mwa wakazi wa kijiji hicho lilitokea majira ya saa 4 asubuhi muda mfupi baada ya msafara wa viongozi hao wa chadema wakiongozwa na aliyekuwa diwani wa kata ya Sombetini jijini Arusha kabla ya kutimkia chadema, Alfonce Mawazo kuwasili kwenye uwanja wa soko la kijiji hicho kwa ajili ya kufanya mkutano wa hadhara wa oporesheni sangara kupitia kauli mbiu yao ya M4C.


Hata hivyo wakati msafara huo ukiwasili kijijini hapo baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo walionekana kuzagaa kila kona na wengine wakicheza mpira ambapo ghafla waliandamana hadi lilipokuwa limesimama gari la viongozi hao wa chadema kisha kulizunguka na kitendo bila kuchelewa walianza kutoa kilio chao kwa viongozi hao wa chadema wakitaka kilio hicho kifikishwe kwa Rais Kikwete.

“Shikamoo..Mmekuja kufanya mkutano hapa…kamwambieni Rais Kikwete hatufundishwi…tunakuja kufanya kazi za walimu na kucheza tukisubili wakati wa kutawanyika na kurudi nyumbani kwetu…walimu wetu wameishia machimboni huko nyangarata”alisikika mmoja wa wanafunzi hao Getruda Shija anayesoma darasa la sita kwenye shule hiyo akilalama huku wenzake wakimshangilia.

Wananafunzi hao,walidai kuwa kwa muda mrefu sasa baadhi ya walimu wa shule hiyo wametimkia machimboni tangu ulipotokea mulipuko wa dhahabu(Gold Rush) katika kijiji cha Nyangarata kilichopo kata ya Butobela Wilayani Geita hali ambayo walidai inawanyima haki yao ya msingi ya kupata elimu bora.

Petro Faida na Emanuel Yohana wanaosoma darasa la tatu katika shule hiyo waliwaeleza viongozi hao wa chadema kuwa,kutokana na walimu wao kutimkia kwenye machimbo hayo kwa ajili ya kuchimba mawe yanayozaniwa kuwa na dhahabu,kwa sasa wamekuwa vibarua wa kufanya kazi majumbani mwa walimu.

“Hapa mnavyotuona tumetoka kufanya shughuli kwa walimu wetu…na tunapumzika kidogo tu tena tunaenda kulima mashamba ya walimu…kamwambieni Rahisi Kikwete tunateseka…hatufundishwi kabisa”alisema Yohana kwa rafudhi ya kisukuma huku akishangiliwa.

Kufuatia hali hiyo,mmoja wa viongozi hao wa Chadema James John na mwandishi wa habari hizi pamoja na baadhi ya wanafunzi hao waliongozana hadi ilipo shule hiyo kwa lengo la kuonana na mkuu wa shule hiyo ili kuthibitisha madai ya wanafunzi hao,ambapo walishangaa kukuta wanafunzi wakiwa wanacheza nje ya madarasa na wengine wamelala vichakani huku mwalimu mmoja akiwa amekaa ofisini.

Mwalimu huyo aligoma kutaja majina yake na hata kuzungumzia madai ya wanafunzi hao kwa madai kuwa si msemaji na badala yake alitoa namba za mkuu wake na kumtaka mwandishi awasiliane naye aliyedai yuko jirani.

Aidha Mkuu wa Shule hiyo John Katabazi mara baada ya kupigiwa simu kisha kukutana na mwandishi wa habari hizi alikiri walimu wake kwenda kwenye machimbo hayo huku akiwatetea kuwa hawafanyi hivyo mara kwa mara.

“Ni kweli hili tatizo lipo…walimu wangu wamekuwa wanakwenda kunusa…wanarudi… kwenye machimbo hayo baada ya kutokea mulipuko wa dhahabu(Gold Rush)..lakini siyo mara kwa mara”alisema Katabazi.

Mbali na hilo,Katabazi alizitaja changamoto nyingine zinazoikabili shule hiyo kuwa ni pamoja na upungufu wa walimu,madawati pamoja na vyumba vya madarasa.


Alifafanua kuwa shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 1192,ikiwa na mikondo 31 inao walimu 12 badala ya 29,na kwamba inayo madawati 188 pekee pamoja na vyumba vya madarasa 7 badala ya 31 jambo alilodai nalo ni kikwazo cha wanafunzi kupata elimu inayowastahili.

Kwa upande wake Mawazo akiwahutubia mamia ya wakazi wa kijiji hicho ambacho ni ngome ya chama cha mapinduzi(CCM)mbali na kuahidi kufikisha kilio cha wanafunzi hao ngazi husika,aliwataka wananchi hao kubadilika kwa kuikataa CCM kwa madai kuwa kuendelea kuchagua pombe,furana,kanga,chumvi na kofia wanazopatiwa na chama hicho hususani wakati wa uchaguzi ndiyo sababu zilizopelekea kijiji chao kukosa huduma muhimu za kijamii.

“Ndugu zangu wana Ntono…maeneo yote waliyochagua Chadema na kuikataa CCM kuna huduma zote za kijamii..ninyi hapa hamna maji..huduma za afya wala miundombinu ya barabara na bado mnachagua CCM hii ni laana… mnakubali kuchagua pombe…furana za kijani…kanga..chumvi na kofia…hivi hamjui wamewafanya kama kuku wa kienyeji…ikataeni CCM mchague mabadiliko”alisema Mawazo.

No comments:

Post a Comment