MPIGA PICHA WA
ITV MKOANI MARA MAXMILLIAN DOMINICK PIA NI MMOJA WA WASHIRIKI KATIKA
MAFUNZO HAYO YANAYOFANYIKA KWENYE HOTEL YA ORANGE TREE.
Na Shomari Binda
Musoma,
WAANDISHI
wa habari wametakiwa kujenga tabia ya kufuatilia bajeti na sera za
halmashauri, ikiwa ni pamoja na kufuatilia miradi inayotekelezwa kwenye
halmashauri husika, ili kuona kama imetekelezwa kwa kiwango
ikilinganisha na fedha zilizotengwa kutokana na bajeti husika.
Rai hiyo ilitolewa jana na
mwanaharakati mmoja Robert Renatus, ambaye ni mwezeshaji kwenye semina
ya mafunzo ya uchambuzi juu ya sera na fedha za serikali, namna
zinavyofanya kazi katika maendeleo ya jamii.
Renatus alisema fedha
nyingi za halmashauri zinazotengwa kwenye bajeti zimekuwa hazitumiki
ipasavyo kwa miradi iliyokusudiwa, ikiwa ni pamoja na miradi mingine
kutekelezwa chini ya kiwango huku fedha hizo zikiwa zimetokana na kodi
ya wananchi.
Mwanaharakati huyo alisema
kuwa kwa jinsi hiyo ni wajibu wa waandishi wa habari kujenga tabia ya
kufuatilia bajeti za halmashauri na kuzipitia kwa kina, ikiwa ni pamoja
na kuona ilivyopangwa, kuhusu makadirio ya mapato na matumizi yake.
“Waandishi wa habari
mnapaswa kufuatilia na kuzisoma bajeti za halmashauri kwa kina ili
muweze kufuatilia utekelezaji wake....nyinyi kalamu zenu ni kitu cha
muhimu sana maana mtaibua vitu ambavyo vimefichika, mtajua mapato na
matumizi, na pia mtafuatilia utekelezaji wa miradi” alisema.
Katika masuala ya
Kisera,Renatus alidai kuzijua Sera mbalimbali za mipango ya Kimaendeleo
ndio itakuwa nafasi nzuri kwa Waandishi wa Habari kuweza kuweza
kuifahamisha Jamii juu ya mipango ya kimaendeleo inayowahusu.
Alisema Wananchi
wanawategemea sana Wandishi wa Habari katika kuwafikishia taarifa
mbalimbali muhimu ili waweze kuzifahamu na kupata nafasi ya kuwahoji
viongozi katika utekelezaji wake.
Wakichangia
kwenye semina hiyo, waandishi wa habari walisema kuwa ufuatiliaji wa
bajeti za halmashauri umekuwa mgumu, kutokana na baadhi ya wakurugenzi
na maafisa mipango kukatalia makaburasha ya halmashauri kwa maelezo kuwa
hizo ni nyara za serikali hazipaswi kupewa raia wa kawaida.
Pia
walisema kuwa pia wamekuwa hawapati ushirikiano wa kutosha kutoka kwa
madiwani, kwa sababu baadhi ya madiwani pia wamekuwa hawasomi
makaburasha hayo na badala yake baada ya kupewa uyaweka makabatini.
Akijibu hoja hiyo,
mwanaharakati huyo alisema kuwa makaburasha ya bajeti za halmashauri ni
kitu cha wazi na hivyo, mwandishi wa habari anayo haki ya kupewa na
kulipitia, ili aweze kujua kulichomo, ambapo atapata fursa ya kuanza
kufuatilia utekelezaji wake.
Aidha alisema kuwa ushiriki
wa wanahabari kushiriki katika mchakato wa bajeti ni mkubwa sana, kwani
watajua dhana nzima ya bajeti, kujua mchakato sahihi wa uandaaji wa
bajeti ya serikali, nani anayeshiriki katika mchakato huo, kujua uhalali
wa vyanzo vya mapato, pamoja na kujua uhalali wa matumizi ya fedha za
umma.
Aliongeza kuwa pia
waandishi watajua thamani ya kulingana na miradi, kutoa elimu ya bajeti
katika lugha sahihi kwa umma, kudhibiti mapato na matumizi kwa kuibua
udhahifu katika utekelezaji wa bajeti na kutoa maoni na mapendekezo ya
maboresho ya bajeti.
Alisema kuwa pia mchakato
mwingine kwa wanahabari ni kulinganisha ufanisi kati ya bajeti na
bajeti, kuhusisha sera na bajeti pamoja vipaumbele vya taifa na
kuboresha upatikanaji sahihi wa taarifa za bajeti na namna ya
kuzitumia.
|
No comments:
Post a Comment