MKANDARASI ADAIWA
KUCHELEWESHA MRADI WA MAJI WA SHILINGI BILIONI 30 BUNDA
Bunda
BAADHI ya wakazi
wa mji wa Bunda na Vijiji vitatu katika halmashauri ya wilaya hiyo mkoani Mara
wameiomba serikali kusitisha mkataba na kampuni ya ujenzi ya Nyakirang’ani
Construction Ltd iliyopewa kazi ya kuchimba
mtaro wa kutoa maji katika ziwa Vctoria kupitia vijiji hivyo hadi mjini Bunda.
Mradi huo mkubwa
wa Maji unaotekelezwa na benki ya dunia kwa ushirikiano na Serikali ya Tanzania
unakusudia kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 30 huku kampuni hiyo ikipewa
kazi ya kuchimba mtaro na kuweka mabomba kwa gharama ya zaidi ya shilingi
bilioni 6.7.
Mji wa Bunda
Wakizungumza na
waandishi wa habari,baadhi ya wakazi hao wa vijiji hivyo vya Guta,Tairo na
Nyantare pamoja na Mamlaka ya mji mdogo wa Bunda walisema kasi ndogo ya
uchimbaji mtaro huo inachangia kutokamilika kwa wakati kwa mardi huo unaotegemewa
na wakazi zaidi ya laki moja katika maeneo hayo
“Wakati mheshimiwa Wassira amekuja kukagua
zoezi la uchimbaji wa Mtaro mkandarasi alionekana kwenda kasi lakini
alipoondoka tu alihamisha vifaa mradi huu hauwezi kukamilika kwa wakati”
alisema Bi Nyanjura Magafu mkazi wa kijiji cha Tairo
Mmoja wa Afisa
katika idara ya Maji mjini Bunda ambaye aliomba kuhifadhiwa jina lake alisema
wakati Stephen Wassira ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Bunda akikagua mradi
huo,Mkurugenzi wa kampuni hiyo ya Ujenzi Mahuza Mmangi alimweleza Mtaro huo ungekamilika ndani ya wiki nne na
kuweka mabomba lakini hadi sasa hakuna dalili za kukamilika kwa Mtaro huo.
“ Ndugu yangu
sisi wengine hapa ni wadogo hatuwezi kulizungumzia hili suala kwa undani,
nadhani huyu jamaa ana watu wanamlinda huko juu ndiyo maana anachelewesha kazi
hii au la sivyo huu umekuwa mtaji wa CCM kwa kuombea kura kwa kila uchaguzi”
alisema Afisa huyo
Alipoulizwa
kuhusu kusuasua kwa mradi huo ambao ni tegemeo kubwa kwa wananchi wa mji wa
Bunda na Vitongoji vyake Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Bunda
Cyprian Oyier alikiri mradi huo kutekelezwa kwa kasi ndogo huku akisema huenda
Mkandarasi ameelemewa na kazi katika Maeneo mengine
“ Hata mimi nashangaa kasi ndogo ya
utekelezaji wa Mradi huu kwani sasa hata mitambo imeondolewa eneo la Mradi
sijui huyu bwana amezidiwa na kazi sehemu nyingine?” alisema Mkurugenzi huyo wa
Halmashauri ya Bunda
Alipotafutwa kuzungumzia
malalamiko hayo Mkurugenzi wa Kampuni ya Nyakirang’ani Bw Mmangi kupitia simu
yake ya mkononi kwa siku tatu mfululizo simu hiyo iliita bila Majibu hata
alipotumiwa ujumbe mfupi wa maandishi ili aweze kufafanua kuhusu malalamiko
hayo hakuweza kujibu.
Mh Wassira akiwa katika eneo la Mradi huo
Mradi huo wa Maji
katika wilaya ya Bunda unatekelezwa na Serikali kupitia Benki ya dunia ikiwa ni
sehemu ya ahadi aliyoitoa Rais Jakaya Kikwete wakati akiomba kura kwa Wananchi
mwaka 2005 kwa ajili ya kutatua tatizo la Maji kwa mji wa Bunda na Vitongoji
Vyake.
Hadi sasa ni wakazi
zaidi ya 20,000 tu kati ya 83,000 wa mji wa Bunda wanaopata huduma ya majisafi na salama na hali
hiyo inachangiwa na uchakavu wa miundombinu ya maji iliyojengwa miaka 40
iliyopita.
No comments:
Post a Comment