”
Nchi ya Kijamaa, iliyojiandaa barabara chini ya Chama, ina nguvu za
Kimaendeleo. Wazembe, wavivu na wapinzani wa nguvu hizo, hupondwa-pondwa
na kusagwa-sagwa wasionekane aateeni!”
Ndugu zangu,
Baadhi
yetu tumepata kuyasikia hayo yakitamkwa redioni enzi za utoto wetu.
Enzi zile za Chama kimoja na redio moja. Zilikuwa ni propaganda
zilizoandamana na vitisho.
Nayo
ni historia yetu, na bahati mbaya, propaganda hizo zimechangia kuifanya
jamii yetu iwe kama ilivyo sasa. Mwaka 2012 bado mwenye fikra tofauti
anaweza kupigwa muhuri wa ’ Mpinzani wa nguvu za kimaendeleo chini ya
Chama na anatakiwa apondwe-pondwe na asagwe asagwe asionekane tena!’
Ndugu zangu,
Umri wangu umenipa bahati ya kuishi kushuhudia baadhi ya matukio makubwa katika nchi yetu. Sisi ndio wale wa ’ Kizazi Cha Azimio’.
Nilikuwa
sijazaliwa, siku ile ya Julai saba,1954 wakati TANU ikianzishwa rasmi
ikiwa na ofisi zake pale Mtaa Lumumba, Kariakoo. Lakini, nilikuwa na
miaka 10 na nilishuhudia kwa macho yangu siku ile ya Jumamosi wakati CCM
ikizaliwa. Ni Februari 5, 1977.
Nakumbuka nikiwa
na watoto wanzangu tulikwenda pale ofisi za TANU Ilala Boma kushuhudia
tukio lile la kihistoria. Nilichoshuhudia pale Ilala Boma ni ’Kuzaliwa
Kwa Chama Kipya’. Niliziona nyuso nyingi za watu wazima zilizojaa
matumaini ya siku zijazo, nasi kama watoto, ujio wa Chama kipya
ulitujengea matumaini ya baadae.
Lakini,
kadri miaka ilivyokwenda, na kwa kusaidiwa na elimu na uzoefu wa
maisha, nimekuwa nikikiona chama kisichofanya mabadiliko ya kimsingi wakati
nchi na jamii ikibadilika kwa kasi. Walau, katika Awamu hii ya JK,
naweza kuona jitihada za makusudi za kujaribu kufanya mabadiliko ndani
ya chama hicho. Hili laweza kuwa jambo la kheri kwa CCM yenyewe na nchi
pia.
Maana,
katika siasa, si wapiga kura tu ndio wenye kuchagua, hata chama nacho
kinachagua. Na chama cha siasa kina mambo mawili tu ya kuchagua;
kubadilika ( kufuatana na wakati) au kufa. Na kwa wakati tulio nao,
chama cha siasa hakiwezi kudumu kwa hila, ghilba na vitisho. Katika
wakati tulio nao, Chama kinachotanguliza matatu hayo kinaonyesha dalili za chama kinachoelekea kaburini. Ndio, miaka ya uhai wake itakuwa inahesabika.
Kuhofiwa haipaswi kuwa sifa ya kiongozi au chama cha siasa. Na ni ukweli, leo kuna Watanzania wenye kukihofia zaidi Chama Cha Mapinduzi kuliko Mungu wanayemwamudu. Na lipi jema kwa kiongozi na chama; kuhofiwa au kupendwa? Mwingine angependa vyote, lakini haiwezekani. Jema ni kupendwa na kuheshimiwa.
CCM
itambue sasa, kuwa, mabadiliko yanakuja hata Tanzania, ni suala la
wakati tu. Na vijana wa Tanzania huenda wasiingie mitaani wakafanya kama
wenzao wa Misri, Tunisia na Libya. Watasubiri siku ile ya kwenda kupiga
kura ifikapo 2015. Hilo la subira ya vijana ndilo tunaloliombea.
Na huku mitaani tunawasikia vijana wengi wa Kitanzania wenye kuisubiri kwa hamu 2015. Yumkini wamedhamiria kuandamana kwa wingi wakiwa na vitambulisho vyao vya kupigia kura. Wataandamana kwenda vituo vya kupigia kura kwa nia ya kuiondoa CCM madarakani kwa nguvu za kura.
Salama ya CCM?
Ni ukweli, kuwa CCM ina hali ngumu kuelekea 2015. Chama kimepoteza mvuto kwa kundi kubwa la vijana. Anayesoma kwa makini alama za nyakati anaweza kuona, kuwa CCM ikiwa na bahati inaweza kwa
tabu kutoa rais 2015, lakini, takribani nusu ya wabunge wa bunge lijalo
watatoka kambi ya upinzani. Na kwa CCM inavyoenenda sasa, itakuwa
miujiza kama rais wa 2020 atatoka CCM.
CCM ijiandae sasa kuwa chama cha upinzani. Na inaweza kubaki hai kwa
muda mrefu kama itaipitisha nchi hii kwenye Katiba itakayoifanya
Tanzania kuwa nchi ya kisasa zaidi. Yawepo mazingira ya uwezekano wa
kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Maana, kwa Katiba ya sasa, CCM ikitoka madarakani, basi, yaweza pia ikawa ndio mwisho wake, kuwa chama hicho kitakufa.
Nimepata kuandika, kuwa ili CCM
isalimike na kubaki madarakani katika chaguzi zijazo, sio tu inahitaji
kufanya mabadiliko makubwa, bali mabadiliko makubwa yenye kishindo.
CCM
inahitaji kurudi kwenye misingi iliyoanzisha chama hicho. Huu ni wakati
wa kurudisha misingi ya kimaadili ya chama na uongozi. Misingi
iliyokuwapo huko nyuma. Angalia, iko wapi Miiko ya Uongozi? Imevunjwa,
na ndio maana ufisadi umetamalaki.
Kwa
MwanaCCM, sasa sio suala la kushinda uteuzi wa ndani ya Chama na
kujihakikishia kuingia Ikulu au Bungeni, kuna umma unaotaka mabadiliko
utakaomkabili mgombea wa CCM, awe mgombea Urais, Udiwani au Ubunge. Kuingia ulingoni na ‘ CCM ile ile’ itakuwa ni hatari kwa wagombea wengi wa CCM siku zijazo.
Ni ukweli, kuwa ndani ya CCM imeanza kuporomoka, misingi iliyopelekea kuanzishwa kwa Chama hicho tukianzia na vyama mama vya TANU na Afro- Shiraz. Hili ni jambo la hatari sana. Ikumbukwe, Vyama mama kwa CCM, TANU na Afro- Shiraz, vilikuwa ni kimbilio la makabwela, kimbilio la wanyonge.
Lakini, CCM ya sasa inakimbiliwa na wafanyabiashara, wasomi na wajanja wengine. Wasomi hapa kwa
maana ya hata wale wenye taaluma zao. Wako tayari kuzikimbia taaluma
zao na kuingia kwenye siasa za vyama, hususan Chama cha Mapinduzi.
Baadhi yao wanasukumwa huko kwa ajili ya kutafuta maslahi zaidi. Maslahi binafsi. Na kuna wanaoambiwa; "Mkitaka mambo yenu yawanyokee, njooni CCM". Si mambo ya wananchi, ni mambo yao binafsi!
.
Kuna wanaokimbilia ndani ya CCM kwa kuamini katika malengo na madhumuni ya kuanzishwa kwa chama hicho. Lakini, kuna wanaokimbilia ndani ya CCM wakiwa na malengo na madhumuni ya kwao binafsi yasiohusiana kabisa na ya CCM. Kwao wao, CCM ni sawa na daraja la miti la kuwasaidia kuvuka na kufika wanakotaka kwenda.
CCM ina nafasi ya kujisahihisha, kama kuna utashi wa kisiasa.
Maggid Mjengwa,
Sweden.
+46 736 966 032
No comments:
Post a Comment