Saturday, August 11, 2012


   VIGOGO WANNE KUFIKISHWA MAHAKANI MARA
 
VIGOGO wanne katika halmashauri ya Musoma vijijini mkoani Mara huenda wakawa ni miongoni mwa watu watakafikishwa mahakamani endapo itathibitishwa kuwa wamehusika katika ubadhirifu wa vocha za ruzuku za pembejeo zenye thamani ya milioni 370.

Vigogo hao ambao wanatajwa kuwa ni wajumbe wa kamati za ugawaji wa vocha hizo pembejea ni mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Nimrod Mkono,aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Musoma Geofrey Ngatuni,mwenyekiti wa halmashauri Magina Magesa na aliyekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Karaine Ole Kunei ambaye kwa sasa ni mkurugenzi wa halmashauri ya Ngorongoro.

Hata hivyo mwenyekiti wa halmashauri ya Musoma vijijini Magina Magesa,aliliambia Nipashe jumapili kuwa katibu wa vikao vya ugawaji wa pembeje hizo ambaye ni mkurugenzi mtendaji,hajawahi kumpa mwaliko yeye na mbunge wa jimbo kama wajumbe halali ili washiriki katika vikao hivyo badala yake wamekuwa wakiwaandikiwa hudhuru katika mahudhurio ya vikao hivyo.

“Ni kweli mimi na mbunge(Nimrod Mkono) kwa nyadhifa zetu ni wajumbe lakini cha kushangaza hatujawahi kupewa taarifa za vikao hivyo hata siku moja lakini katika mahudhurio wametuandikia tumeomba hudhuru wakati hatujawahi kuitwa wala hatujui vikao hivyo…hapa anaejua suala hili ni katibu lakini mimi na mbunge hatumo”alisema Magina.

Tuhuma za ubadhirifu huo ziliibuliwa katika baraza la madiwani lilofanyija juzi mjini hapa baada ya madiwani kukataa kupokea taarifa za upokeaji na ugawaji wa vocha hizo za pembejeo za kilimo baada ya kubaini kuwa hakuna pembejeo ambazo zimewahi kufikishwa kwa wakulima wa halmashauri hiyo katika msimu wa kilimo wa mwaka 2011/2012.

Uamuzi huyo umefikiwa katika kikao  hicho cha kawaida cha baraza hilo chini mwenyekiti wake  Magina Magesa,ambapo kwa pamoja madiwani hao baada ya kukataa  taarifa hiyo wameunda tume ya watu sita ili kuchunguza tuhuma hizo.

Wakizungumza kabla ya kuundwa kwa tume hiyo,baadhi ya madiwani hao bila kujali itikadi za vyama vyao,wamedai kuwa hakuna hata kijiji kimoja cha halmashauri hiyo kilichowahi kupokea pembejeo hizo za kilimo kama taarifa hiyo ilivyonyesha huku ikitaja kuwa ununuzi wa pembejeo hizo umeigharimu serikali kiasi hicho cha fedha.

“Mimi nilipata taarifa za kuletwa vocha za ruzuku kutoka kwa mkuu wa mkoa eti halmashauri yetu ililetewa vocha za milioni 370 lakini ukweli ni kwamba hakuna vocha iliywahi kuletwa katika kata yangu…naungana na wenzangu tuunde tume kuchunguza tuhuma hizi za wizi ili ikibainika wahusika wafikishwe mahakamani mara moja”alisema diwani wa kata ya Tegeruka Alpha Mordekai.

Naye diwani wa kata ya Mugango Wandwi Kunju,alisema upotevu wa pembejeo hizo ni miongoni mwa tuhuma nyingi za ubadhifu wa fedha za serikali katika halmashauri hiyo jambo lilokwamisha utekelezaji wa miradi mingi ya maendeleo mingine ikitekelezwa chini ya kiwango hivyo kutaka baada ya tume hiyo kutoa majibu yake watuhumiwa wafikishwe katika vyombo vya sheria kwaajili ya kuwatendea haki wananchi.

Kwa upande wake akizungumza katika kikao hicho,mwenyekiti wa halmashauri hiyo Magesa,alisema kitendo ambacho kimefanywa na idara ya kilimo katika kitengo cha vocha za ruzuku za pembejeo,licha ya kuwa ni cha hujuma kubwa kwa wakulima,maendeleo ya halmashauri hiyo pia kitafanya wananchi kukichukia chama cha mapinduzi na serikali yake endapo hatua za kisheria hazitachukuliwa dhidi ya wahusika baada tume hiyo kuwasilisha taarifa yake.

“Kwa mazingira haya kweli watanzania tutafika hivi hapa ndo kusema CCM inawaletea neema wananchi..lazima tuchukiwe iwe ccm,serikali na halmashauri yenyewe huu ni wizi wa kutisha kama kweli kila diwani hajawahi kupokea pembejeo hata mimi ni mjumbe sijawahi kuitwa katika kikao cha kugawa sasa tunakwenda wapi!kumbe ndio maana mkuu wa mkoa alisema hawezi kuleta chakula cha msaada kwetu kwa vile alijua tumeiba vocha za pembejea,kwa kweli lazima hatua zichukuliwe ili kuinusuru serikali ya chama chetu”alisema Magina.

Hivi karibuni mkuu wa mkoa wa Mara John Tupa,alibaini baadhi ya halmashauri katika mkoa wa Mara kutumia vibaya vocha za pembejeo za ruzuku zingine zikiuzwa nje ya nchi huku wakitumia wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari kusaini katika vitabu maalum vya kupokelea vocha hizo kwa kuwafanya ni wakulima ambao walistahili mgao huo.

Wakati huo huo mgogoro mkubwa umelikumba baraza la Madiwani katika halmashauri ya Musoma vijijini mkoani Mara hadi kufikia baadhi ya madiwani kutaka kupigana baada ya madiwani wa tarafa ya Nyanja kupinga mgawanyo wa halmashauri hiyo ili kuwa halmashauri mbili.

Mgogoro huo ulikuja juzi baada kutokea tena hivi karibuni katika kamati ya fedha na mipango jambo lilosababisha kuvunjika kwa kikao hicho na kupeleka hoja hiyo katika kikao cha chama cha mapindizi ccm kabla kurudishwa juzi katika baraza hilo.

Hali hiyo imetokea katika baraza la kawaida madiwani kufuatia  Serikari kutaka kuanza mchakato wa kugawa halmashauri hiyo ili moja ya halmashauri hiyo iwe ya Butiama baada ya kupatikana kwa wilaya mpya ya Butiama.

Wakizungumza katika kikao hicho kabla ya madiwani wa kata kumi na saba kati ya 34 kutoka wa tarafa ya Nyanja bila ya kujali itikadi zao za vyama vya siasa kutoka nje ya ukumbi,walisema kitendo cha kugawa halmashari hiyo huku ikiwa chini ya utawala wa wilaya ya Butiama hakitawatendea haki wananchi.

“Hutuwezi kukubali kuwa chini ya mkuu wa wilaya ya Butiama kwani kufanya hivyo ni kutowatendea haki wananchi…mwananchi hawezi kutoka Busekera hadi Butiama zaidi ya kilometa 200 kumtafuta mkuu wa wilaya wakati mkuu wa wilaya ya Musoma anaweza kumuona kwa kutembea kilometa 50 tu jambo hili hatukabali hata kidogo”alisema diwani wa Busekera katika kikao hicho Mambo Rebule akiwa miongoni mwa madiwani 17 wa tarafa ya Nyanja baadhi ya kata za tarafa ya Makongoro walipinga hoja hiyo na kutoka nje ya ukumbi

Aidha waliongeza kuwa Jografia ya tarafa ya Nyanja itawafanya wananchi kushindwa kupata huduma mbalimbali za kwa viongozi wa wilaya ya Butiama kutokana na umbali huo uliopo huku wakisisitiza kuwa jambo hilo linapaswa kuangaliwa upya ikiwa ni pamoja na kuendelea kuwa chini ya mkuu wa wilaya ya Musoma.
 
Hata hivyo baada ya madiwani hao kutoka nje ya ukumbi,baadhi ya madiwani wa tarafa za Makongoro na Kiagata wote  wa chama cha mapinduzi,walipendeza kugawa halmashari mbili kwa kuwa na kata ya kumi na saba kila moja huku halmashauri ya Nyanja ikipendekezwa kujengwa eneo la Kwikonero kata ya Suguti,mapendekezo ambayo sasa yatafikishwa katika kikao cha ushauri cha mkoa RCC.

No comments:

Post a Comment