Monday, June 16, 2014

Serikali yakabidhiwa `chopa` kupambana na ujangili

Na Beatrice Shayo
15th June 2014



Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu (wa pili kutoka kushoto) akikabidhiwa funguo ya `chopa` ya kupambana na majangiri na rubani Mkuu na Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya helikopta ya Marekani, Peter Achammer.
 
Jitihada za kupambana na ujangili zimepata nguvu zaidi, baada ya serikali kukabidhiwa helikopta ya kufanya doria kwenye hifadhi za wanyama pori na maeneo ya mapori tengefu.

Serikali imeungwa mkono na taasisi ya Howard Buffett Foundation ya Marekani, iliyomkabidhi Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, helkopta yenye thamani ya Dola 500,000 sawa na Sh milioni 800.

Msaada huo uliokabidhiwa jana na Balozi wa Marekani nchini Childress Mark ,kwa niaba ya taasisi ya Marekani ya Howard Buffett Foundation.

Nyalandu alisema kuwa helikopta hiyo imetolewa kwa ajili ya kupambana na ujangili huo.

Waziri  Nyalandu alisema taasisi ya Howard Buffett Foundation ambayo inaratibiwa na Mark Rigel aliunga mkono jitihada za kupambana na ujangili na kumuahidi Rais Jakaya Kikwete, kutoa msaada wa kupunguza changamoto hiyo.

Pia alisema waliahidi kutoa Dola 500,000 (sawa na Sh 800)na anatumaini kuwa endapo fedha hizo zitatolewa zitatumika katika masuala ya kupambana na ujangili.

Nyalandu alisema maisha ya baadaye ya wanyama  yanategemea jitihada za ulinzi, sambamba na  wananchi wanaoishi kandokando ya hifadhi, hivyo vijiji hivyo vinahitajika kupewa motisha itakayowawezesha kulinda hifadhi hizo.

Alisema wizara inatumia njia za kila aina kuwalinda wanyamapori ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kama ilivyo kwa Howard Buffett Foundation.

Balozi Mark alisema jitihada za pamoja za wadau wa ndani na nje zinahitajika kupambana na ujangili na majangili na kwamba vitu vingine muhimu ni pamoja na wafanyakazi na vitendea kazi.

Akizungumza katika makabidhiano hayo Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa (Chadema) Iringa Mjini, alisema tukio hilo ni la muhimu na kwamba tayari waziri Nyalandu alishaahidi bungeni.

“Naamini itasaadia katika vita hiyo ya ujangili,kwani kwa muda mrefu tumekuwa tukipigania suala la ujangili hivyo tumefurahia kilio chetu kusikika” alisema Msigwa.

No comments:

Post a Comment