KAMATI
ya Uchaguzi ya Simba SC imesema kwamba, Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF) halina mamlaka kikatiba kusimamisha uchaguzi wa klabu hiyo, na
maana yake uchaguzi huo upo kama ulivyopangwa kufanyika Juni 29, mwaka
huu.
Pamoja na hayo, Kamati hiyo imesema imemuondoa moja kwa moja mgombea
Michael Richard Wambura kwenye kinyang’anyiro hicho kwa sababu amerudia
kosa ambalo aliwahi kupewa onyo.
SOMA:
TAARIFA KAMILI YA NDUMBARO;
Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club, ilifanya mkutano wake kawaida
tarehe 15 Juni 2014 kujadili mambo mbalimbali ambayo yanayohusu uchaguzi
mkuu wa Simba Sports Club ambao umepangwa kufanyika tarehe tarehe 29
Juni 2014. Kamati ya Uchaguzi ya Simba sports Club inapenda kuujulisha
umma, hususan wapenzi wa Simba Sports Club mambo yafuatayo:
1. Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club, kwa mujibu wa Ibara ya 10(6)
ya Kanuni za uchaguzi za TFF toleo la mwaka 2013, ndiyo chombo pekee
chenye mamlaka ya kutangaza, kubadilisha, kusimamisha au kufuta tarehe
ya Uchaguzi ya Simba Sports Club. Kwakuwa Kamati haijafanya hivyo, wala
hakuna mdau yoyote aliyeleta hoja ya kusimamisha uchaguzi,
tunawajulisha kuwa uchaguzi wa Simba Sports Club upo pale pale kama
ambayo Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ilivyopanga. Maandalizi
ya uchaguzi huo yanaendelea vema na Uchaguzi utafanyika tarehe 29 Juni
2014 kama ilivyopangwa hapo awali.
2. Kamati imesikia kupitia vyombo vya habari kuwa TFF imesimamisha
uchaguzi wa Simba Sports Club mpaka hapo Kamati ya Utendaji ya Simba
Sports Club itakapoteua Kamati ya Maadili. Kamati ya Uchaguzi ya Simba
Sports Club inapenda kusema yafuatayo:
i. Mamlaka ya kusimamisha uchaguzi ni kazi ya Kamati ya Uchaguzi ya
Simba Sports Club kwa mujibu wa ibara 10 (6) ya Kanuni za Uchaguzi, 2013
ii. Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ilipoanza mchakato wa
uchaguzi ilitoa tamko kuwa: “kwasababu Simba Sports Club haina kanuni za
Uchaguzi, Kamati ya Rufaa ya uchaguzi, wala Kamati za Maadili kwa
mujibu wa ibara za 16 (e) na (f) ya Katiba ya Simba Mwaka 2014, vyombo
husika vya TFF vitatumika”. Kulikuwa hakuna pingamizi toka kwa mtu
yoyote juu ya kauli hiyo, ikiwemo TFF.
iii. Tarehe 26 Mei 2013, Rais wa TFF aliialika Kamati ya Uchaguzi ya
Simba Sports Club katika chakula cha mchana. Katika mkutano huo, kauli
ya aya (ii) hapo juu ilirejewa na Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports
Club ilikabidhi rasmi mchakato mzima wa uchaguzi na kutoa ufafanuzi kuwa
kamati husika za TFF zitahusika, jambo ambalo halikupingwa na TFF.
iv. TFF iliruhusu Kamati ya Rufaa ya Uchaguzi ya TFF kusikiliza Rufaa za
uchaguzi za Simba, hivyo basi haiwezi kuzuia Kamati zake nyingine
kusikiliza Masuala ya kimaadili. “Estopel” inawazuia TFF kufanya hivyo
sasa.
v. Wajumbe wote wa Kamati ya Utendaji ya Simba Sports Club, isipokuwa
watatu tu, ni wagombea katika uchaguzi huu. Na hao watoto tayari wapo
kwenye Kambi za Kampeni za uchaguzi hii ambazo zipo bayana kabisa.
Kuiagiza Kamati ya Utendaji ya Simba iunde Kamati ya Maadili kusikiliza
kesi za maadili dhidi yao wenyewe ni kukiuka msingi wa haki ya asili
(natural justice). Ni dhahiri kuwa haki haiwezi kutendeka kwa wajumbe wa
kamati ya utendaji ya Simba Sports Sports Club, ambao ni watuhumiwa
katika masuala ya maadili, wachague majaji wa kuwahukumu. Hapo haki
haitatendeka.
Ifahamike kuwa, baada ya Kamati ya Utendaji ya Simba Sports Club kuteua
Kamati ya uchaguzi ya Simba Sports Club, Kamati hiyo haina mamlaka tena
ya kujadili, kuingilia au kuteua chombo kingine kufanya shughuli
zinazohusu uchaguzi ukizingatia kuwa wajumbe wake ni wagombea.
vi. Katika Uchaguzi Mkuu wa TFF wa Mwaka 2013, ambao ulimuingiza Jamal
Malinzi Madarakani, FIFA walikuja, wakongea na pande zote na hatimaye,
walisema kuwa; “tunapendekeza kuwa uchaguzi mkuu usimame ili kuunda
kamati mbalimbali”. Mapendekezo hayo yalipokelewa na Kamati ya Uchaguzi
ya TFF, Bw. Deo Lyato, na hatimaye ni Kamati ya Uchaguzi ya TFF ndio
iliyotangaza kusimamisha Uchaguzi na sio Sepp Blatter.
vii. Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ni Kamati huru ambayo
haipaswi kuingiliwa na Chombo chochote kile. Ili kulinda uhuru huo,
tunalazimika kukanusha matamshi ya TFF kuhusu kusitisha Uchaguzi Mkuu wa
Simba Sports Club.
3. Malalamiko ya Kimaadili Kupelekwa FIFA.
Kwa mujibu wa Ibara ya 11 (9) ya Kanuni za Uchaguzi za TFF, 2013, inatoa
mamlaka kwa Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club kupeleka masuala
ya maadili katika kamati ya maadili ya TFF. Tarehe 9 Juni 2014, Kamati
ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ilipeleka Masuala ya Maadili katika
Kamati ya Maadili ya TFF. Kwakuwa TFF imekataa kusikiliza masuala ya
maadili ambayo yanakiuka Kanuni za maadili, Katiba za Simba, TFF na
FIFA, Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club, itapeleka Masuala ya
Maadili FIFA ili haki itendeke.
4. Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ilijadili kuhusu vitendo vya
wagombea kupiga kampeni kabla ya muda wa kampeni ulioruhusiwa. Kwa
mujibu wa Mchakato wa Uchaguzi ya Simba Sports Club, muda wa kampeni
unaanza tarehe 24 -28 Juni 2014. Hapo awali kamati ilibaini kuwa
wagombea wawili wa nafasi ya urais; Michael Richard Wambura na Evans
Aveva walifanya vitendo vya kampeni siku ya kuchukua na kurejesha fomu
za kugombea. Tarehe 25 Mei 2014, Kamati iliwapa ONYO KALI la maandishi
wagombea hao na kuwataarifu kuwa hatua kali zaidi zitachukuliwa dhidi
yao, ikiwemo kuondolewa katika kinyang’anyiro cha uchaguzi.
Baada ya Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club kumuondoa Bw. Michael
Richard Wambura katika kinyang’anyiro cha uchaguzi Mkuu wa SImba Sports
Club, Bw. Wambura aliitisha Mkutano na waandishi wa habari, aliitukana
Kam
ati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club, na kutoa matamshi ambayo ni Kampeni.
Baadaya ya Kamati ya Rufaa ya uchaguzi ya TFF kumrejesha Bw. Wambura
katika Kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa Simba, Bw. Wambura aliitisha
tena mkutano wa waandishi wa habari, aliisifu kamati ya Rufaa ya
Uchaguzi ya TFF, kwa mara kwanza aliisifu Kamati ya Uchaguzi ya Simba
Sports Club na kutoa matamshi ambayo ni wazi kuwa ni kampeni. Baadhi ya
Matamshi aliyoyatoa kupitia vyombo vya habari ni kama ifuatavyo:
i. “Simba Sports Club inahitaji zaidi wadhamini na sio wafadhili”
ii. “Wafadhili kazi yao in kutoa fedha mfuko wa kushoto na kuepeleka mfuko wa kulia”
iii. “Simba ilikuwa na viwanja vitatu lakini kimoja kimeuzwa na wajanja na vimebaki viwili tu”
Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ilitafakari matamshi hayo, na
kubaini kuwa hiyo ni kampeni ya waziwazi wakati muda wa kampeni bado
haujaanza.
Kamati ya Uchaguzi ya Simba Sports Club ililipa jambo ili uzito wa
kipekee kwasababu Mkosaji amekuwa na tabia ya kurudia kosa hilo hata
baada ya kupewe onyo la maandishi.
HIVYO BASI:
Kwa mujibu wa mamlaka ya kikanuni, hususan Ibara za: 6 (1) (a) – (g); 6
(1) (L) na 14(3) za Kanuni za uchaguzi za TFF – 2013, Bw. Michael
Richard Wambura anaondolewa Katika Kinyang’anyiro cha Uchaguzi wa Simba
Sports Club, 2013, kwa kosa la kurudia kufanya kampeni kabla ya muda
wa kampeni ambao umepengwa,".
No comments:
Post a Comment