Wednesday, June 18, 2014

Wahariri 25 wa habari wanufaika na Mafunzo kutoka THRDC

Wahariri 25 kutoka vyombo mbali mbali vya habari vikiwamo magazeti, redio, televisheni na hata mitandao ya kijaamii Tanzania Bara na Visiwani (Zanzibar) wamenufaika na mafunzo ya usalama kutoka kwa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC). 

Mafunzo hayo ya siku tatu yaani tarehe 13 hadi 15 Juni, yalitolewa na wakufunzi wa ndani ya taasisi Bw. Onesmo Olengurumwa ambaye ni mratibu wa THRDC na Bw. Elias Mhegera ambaye ni afisa habari katika mtandao huu. Wengine waliotoa mada ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitengo cha habari Dk. Ayub Rioba, na mshauri mwelekezi, ambaye pia ni mhariri mkongwe Bw. Rweyemamu kutoka New Habari 2006 Ltd.

Miongoni mwa wahariri walitoka mikoani kama vile Mbeya, Arusha, Kigoma, Zanzibar n.k. usawa wa kijinsia ulizangatiwa katika utoaji wa mafunzo hayo. Mada zilizofundishwa ni pamoja na namna ya kuchukua tahadhari katika utekelezaji wa kazi za uandishi, namna ya kung’amua na kutathmini tishio la kiusalama, namna ya kutunza taarifa katika njia salama na maadili ya kitaaluma katika fani ya habari.

Aidha Dk. Rioba alizungumzia hatari zinazowakabili waandishi wa habari za uchunguzi na namna ya kukabiliana nazo. Mafunzo hayo yalitumika pia katika kujadili changamoto mbali mbali wanazokutana nazo wahariri na hata falsafa mbali mbali zinazoleta mikinzano katika utendaji wao wa kazi. Hii ni pamoja na mitazamo ya kiitikadi, sheria zinazobana uhuru wa habari na hata maslahi kinzani ya wamiliki wa vyombo vya habari. 

No comments:

Post a Comment