Tuesday, April 15, 2014

Makachero wa Polisi Zanzibar wakamata Silaha zilizotumika katika Mauaji ya Akari Polisi


Makachero wa Jeshi la Polisi Zanzibar, wamefanikiwa kuzikamata silaha mbili na risasi 40 za Kivita zinazosadikiwa kutumika katika matukio mbalimbali ya kihalifu likiwemo la mauaji ya Askari Polisi lililotokea Machi 2, mwaka huko kwenye Hoteli ya Kitalii ya Pongwe Bay mkoa wa Kusini Unguja Zanzibar.

Taarifa ya Afisa habari Mkuu wa Jeshi la Polisi Zanzibar Inspekta Mohammed Mhina, imemkariri Mkurugenzi wa Upelelezi Zanzibar SACP Yusufu Ilembo, akisema kuwa pamoja na kukamatwa kwa silaha hizo pia Makachero hao wamewatia nguvuni majambazi watatu kati ya wanne waliohusika katika tukio hilo la mauaji ya Polisi.
Mapema akizungumza na Waandishi wa Habari mjini Zanzibar SACP Yusufu  Ilembo, alisema silaha hizo zilikamatwa nyumbani kwa mmoja wa watuhumiwa anayeishi eneo la Mkokotoni katika mkoa wa Kaskazini Unguja zikiwa zimefungwa na vipande vya plastiki na vitambaa na kuviringishwa katika waya mpya wa kupigilia madirisha.
Bila ya kuwataja majina yao kwa sababu za kiupelelezi, DCI Ilembo ameainisha wazi kuwa baadhi ya watuhumiwa hao ni wenyeji wa Pangani mkoani Tanga na wengine ni wenyeji wa Kisiwa cha Pemba Zanzibar.
Amesema katika mahojiano na makachero wa Polisi, Majambazi hayo pia yalikiri kuhusika na matukio mbalimbali katika mikoa ya Viisiwani na Mikoa ya Tanzania Bara matukio ambayo yangali yakichunguzwa katika Vituo mbalimbali vya Polisi.
Watuhumiwa hao pia walipatikana na vitu mbalimbali zikiwemo fedha taslimu shilingi 490,000 za Kitanzania, dolla 75 za Kimarekani, Euro na fedha kadhaa za Kichina pamoja na vitu mbalimbali zikiwemo simu za mkononi.
Hata hivyo, SACP Ilembo amekiri wazi kuwa kukamatwa kwa silaha hizo pamoja na watuhumiwa, kumetokana na taarifa za siri za Raia wema zilizotolewa Polisi na kupelekea kufanyiwa kazi na kuleta mafanikio hayo.
Amewaomba wananchi katika maeneo mbalimbali kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za siri zitakazowafichua watuhumiwa wakiwemo waliofanya na wanaotarajia kufanya makosa ili waweze kufuatiliwa na kukamtwa na kufikishwa mahakamani kwa hatua zaidi.
 

No comments:

Post a Comment