Saturday, June 22, 2013

NHIF YAWAKUMBUKA MPANDA KATAVI YAPELEKA MADAKTARI BINGWA

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Emanuel Humba.


Na Grace Michael
MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya unaendelea kutekeleza mpango wake wa kuhakikisha utaalam wa madaktari bingwa wachache waliopo hapa nchini unatumika kitaifa na unawanufaisha Watanzania wote.
Kutokana na hali hiyo, timu ya madakati bingwa saba na watalaam wengine wawili itaanza kazi rasmi katika Mkoa wa Katavi siku ya Jumatatu katika Hospitali ya Mpanda na timu hiyo itahudumia wananchi na wanachama wa Mfuko kwa muda wa siku saba.

Mbali na kutoa huduma katika Mkoa mpya wa Katavi, timu hiyo pia ianatarajiwa kutoa huduma katika Mkoa wa Rukwa mapema Julai na itadumu kwa muda wa siku saba lengo ni kutoa huduma hizo za kitaalam kwa wananchi hao ambao kwa muda mrefu wamekosa fursa hiyo.

Akizungumza na timu hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Emanuel Humba alisema kuwa lengo la Mfuko kugharamia mpango huo ni kuhakikisha utaalam wa madaktari bingwa ambao ni wachache hapa nchini unatumika kitaifa.

“Kwanza niwashukuru sana madaktari kwa kukubali kushirikiana na sisi, inatupa nguvu ya kuendelea na mpango huu lengo kubwa ni kuwahudumia wananchi wote bila ya ubaguzi…wananchi na wanachama watatakaokuwa na mahitaji ya kuonana nanyi Nawaomba sana muwahudumie kwa kadri ya utaalamu wenu ili kila mwananchi anufaike na uwepo wenu kwa muda mtakaokuwa huko,” alisema Bw. Humba.

Alisisitiza kuwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya mbali na mpango huo utaendelea na mikakati mingine ya kuhakikisha inashiriki kikamilifu katika uboreshaji wa huduma za afya lakini pia kuwasaidia wananchi kutambua afya zao mapema kupitia mpango wa elimu kwa umma utakaokwenda sambamba na upimaji wa afya bure kwa wananchi.

Timu ya Madaktari hiyo ni pamoja na Dr. Billy Aonga (bingwa wa Mifupa), Dr. Albert Ulimali (bingwa wa Usingizi), Hillary Tesha (Mtalaam wa Mazoezi tiba) na July Nkwama (Mhudumu wa Chumba cha upasuaji) wote kutoa Taasisi ya Mifupa (MOI). 
Wengine ni Dr Delila Kimambo (Bingwa wa magonjwa ya kawaida na moyo), Dr. Edna Majaliwa (bingwa wa watoto) wote kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Timu hiyo pia itajumuisha na Daktari bingwawa upasuaji kutoka Hospitali ya Rufaa Mbeya na Daktari bingwa wa magonjwa ya akina mama na kawaida kutoka hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Rukwa.

Kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Mwenyekiti wa Bodi Balozi Ally Mchumo, Mjumbe wa Bodi, Bi Lyidia Choma na Mkurugenzi Mkuu.

No comments:

Post a Comment