Sunday, June 23, 2013

ASKARI WANYAMAPORI WATUHUMIWA KUZAMISHA NG’OMBE 51 MTONI NA WENGINE 100 KUPOTEA.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mariwanda wilayani Bunda  Samson Kisung’uda


Juni 22,2013.
Mara-ASKARI  wa mapori ya akiba ya Ikorongo na Grumeti  kwa kushirikiana na Kampuni ya Singita Game Reserve ,wanatuhumiwa kusababisha vifo vya  ng’ombe 51na 100 kupotea wa mkazi mmoja wa Kijiji cha Mariwanda wilayani Bunda.
 
Tukio hilo linadaiwa kutokea aprili 22,majira ya saa 10.30 jioni mwaka huu katika eneo la Mto Rubana eneo la Mariwanda limethibitishwa na polisi na ofisi ya mifugo wilaya ya Bunda na uongozi wa kijiji hicho.
 
Kiteku Meshinya Kisereta mwenye mifugo akiongea na Mwandishi wa blog hii katika ofisi ya Wasaidizi wa Kisheria na Haki za Binadamu wilayani Serengeti (WASHEHABISE)alisema,chanzo cha vifo hivyo ni askari hao waliowakamata kwa kuingia hifadhini kuwasagwa na kuwazamisha mtoni ili wavuke na kufa 51,na wengine 100 hawajaonekana.
 
“Mizoga iliyoopolewa majini 51 na kuthibitishwa na polisi na ofisi ya mifugo…wengine 100 haijulikani walikopotelea..,siku hiyo nilitaarifiwa kupitia simu namba 0682 760012,0756 019672 na 0786 757603,kuwa ng’ombe wangu wamekamatwa na askari wa Grumeti nikalipe faini…wakati najiandaa kwenda nikataarifiwa na mchungaji wangu kuwa wamezamishwa mto Robana”alisema.
 
Alisema alilazimika kujulisha uongozi wa kijiji ,mkuu wa wilaya ya Bunda akamtuma Oc Cid ambapo walifika na kukuta ng’ombe 46 wamekufa maji,na aprili 24 walipata mizoga 5 na kufanya idadi ya 51,lakini wengine 100 haikujulikana wako wapi na hakuwahi kuwapata.
 
“Si mara ya kwanza ng’ombe wangu kukamatwa kutokana na shida ya maji wanajikuta wamevuka…askari hupiga simu ama wanasema tuma fedha ya faini kwa Mpesa…ukilipa wanaachiwa ingawa hawatoi stakabadhi….hata siku hiyo walinipigia niende na fedha,ajabu wakaamua kuwasukumia mtoni baada ya kuchelewa,”alisema kwa masikitiko.
 
Aliwataja askari waliohusika na tukio hilo kuwa ni Peter Gorobani na Juma Mwiyuga askari wa Kampuni ya Singita Grumeti Reserves,ambao walikuwa chini ya uongozi wa   Anthony Mamboleo wa Pori la Ikorongo ambaye yuko chini ya Mkurugenzi wa wanyamapori.
 
Serikali ya Kijiji 
Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mariwanda Samson Kisung’uda alisema tukio hilo ni mwendelezo wa Manyanyaso wanayopata wananchi dhidi ya mwekezaji na wizara,”wananchi wamefikia hatua mbaya maana hawa mwaka juzi walifukuza kijana aliyekuwa anachunga ng’ombe akazama mtoni akafa,hakuna hatua zilizochukuliwa dhidi ya wahusika”alisema.
 
Alisema mambo kama ya Mtwara huenda yakajitokeza kwa kuwa wananchi wanahasira na kampuni ya Singita Grumeti Reserves kutokana na vijana wake wanavyowatendea unyama wananchi,”sisi viongozi tunapata shida sana…siku hiyo ilikuwa wanaungana na vijiji vya jilani kwenda kuteketeza magari yao….tulitumia ushawishi kuwatuliza …kukaa kimya bila watakuja shangaa”alibainisha.
 
Kutokana na ukubwa wa tatizo waliwasiliana na Mbunge wa jimbo hilo Steven Wasira ambaye ni Waziri ofisi ya Rais Uhusiano na kuagiza kuandika barua kwenda kwa waziri wa Maliasili na Utalii ili aweze kuchukua hatua.
 
Barua hiyo ya mei 10,2013 imefafanua ilivyotokea na kunakilishwa kwa viongozi mbalimbali ,akiwemo mkuu wa mkoa wa Mara ,mbunge.Rpc,Dc na Ocd Bunda kwa Taarifa,hata hivyo hawajapata majibu kutoka wizara licha ya Mbunge wao kuwahakikishia kuwa alimkabidhi waziri mwenye dhamana.
 
Watuhumiwa.
Anthony Mamboleo askari wa pori la Ikorongo alipoulizwa kwa njia ya simu,alikiri kuwepo kwa tukio hilo,lakini hakutaka kulizungumzia”naomba umtafute kaimu meneja wa Ikorongo akupe taarifa zaidi”alisema na kukata simu.
Juma Mwiyuga(askari wa Singita Grumeti game reserves(VGS)alisema yeye alishatoa maelezo polisi ilivyotokea ,”kwanza nilikuwa post sikuwepo…lakini nilishatoa maelezo polisi…haya mambo mimi sipendi kuyazungumzia zaidi”alijibu.
Peter Gorobani alipoulizwa alisema hilo suala hawezi kulisemea mpaka afuatwe ofisini kwake atasema mambo mengi,alipoulizwa ofisi yake ilipo ili blog imtafute  akasema”sasa unataka kuja ofisini….aaah,kwaheri”akakata simu.
 
Kaimu Meneja Ikorongo.
Upendo Kimaro kaimu Meneja mapori ya akiba ya Ikorongo na Grumeti alipoulizwa kuhusu tukio hilo alikiri kuwepo lakini akasema kuna anayeshughulikia”sisi tunafanya kazi chini ya Kanda tunatoa taarifa Kikosi cha Kuzuia Ujangili (KDU)wanasema suala hilo liko Mahakamani tafuta katibu Mkuu ama Mkurugenzi wa wanyama pori watalisemea maana tunawashitaki sisi”alisema. 
 
Hata hivyo suala hilo halijafikishwa mahakamani kama alivyodai meneja huyo ,alipotakiwa kueleza jalada lipi liko mahakamani kwa kuwa jalada la polisi BND/INQ/22/2013 lililofunguliwa na Meshinya dhidi yao halijafikishwa mahakamani,alisema”basi litakuwa polisi…maana nasi tuliwashitaki”alisema bila kutaja mashitaka hayo.
 
Mkurugenzi akana hana taarifa.
Mkurugenzi wa Wanyamapori Tanzania Alexander Songorwa alipoulizwa kwa njia ya simu kuhusu malalamiko ya mfugaji huyo alisema hana taarifa,”wewe ni Mwandishi wa pili ,juzi nimeulizwa kwa kweli sina taarifa nafuatilia nitajulisha kama kuna maandishi yoyote yameletwa na mtu wetu wa huko”alisema.
 
Hata hivyo alijibu kwa ujumbe mfupi wa simu(sms)kuwa hakuna taarifa iliyowahi wasilishwa kwake na maafisa wake kama walivyodai.
 
Ofisa Mifugo akiri.
Masuke Ogwa ofisa mifugo wilaya ya Bunda kupitia simu ya Mkurugenzi mtendaji halmashauri ya wilaya ya Bunda Simon Mayeye alikiri kushuhudia mizoga ya ng’ombe na kuwa walikufa maji,”mazingira yaliyopelekea wafe ni kazi ya polisi…lakini kwa ujumla nilishuhudia ng’ombe kama 51 au 52 wamekufa na ripoti ipo nitaikabidhi polisi “alisema
 
Singita.
Afisa mahusiano wa Kampuni ya Singita Grumet Game Reserves Shaabani Madanga alisema analifahamu suala hilo,na mlalamikaji amelifikisha kwa Waziri,”hata hivyo kwa huko linashughulikiwa na Ikorongo Game Reserves”alisema.
 
Wanaharakati.
Mwenyekiti mtendaji wa shirika la Wasaidizi wa Kisheria na Haki za Binadamu wilaya ya Serengeti Samweli Mewama alisema ,uwekezaji unaowatia umaskini wananchi huibua hasira na chuki na kuomba serikali kuchukua hatua ili mfugaji atendewe haki.
 
Mtandao wa wafugaji ,warina asali na waokota matunda(Ping’os)walisema wanafuatilia tukio hilo ili kuhakikisha mwananchi huyo anatendewa haki,kwa mazungumzo ama mahakamani.
 
Waziri
Juhudi za kumpata Waziri wa Maliasili na Utalii Khamisi Kaghasheki hazikuzaa matunda baada ya simu yake kuita bila kupokewa,na hata alipotumiwa maswali kutaka kujua hatua gani imechukuliwa,licha ya kupokelewa lakini hakujibu.
 
Matukio Mengine.
Blog hii  imebaini oktoba 8,2008 askari wa Ikorongo na Kampuni ya Singita Grumeti Reserve aliswaga ng’ombe kwa kutumia magari na kusababisha ng’ombe  65  mali ya Gorobani Marosina mkazi wa Issenye wenye thamani ya sh,24,600,000 kuzama Mto Robana na kufa na kuthibitishwa na Paulo Munkhoma Augustine afisa mifugo na taarifa yake yenye kumb.Na.Vy/a.20/1/30 kwenda kwa Dc ikionyesha tathimini aliyotakiwa kulipwa .
 
Hata hivyo licha ya Tathimini kuonyesha alivyostahili kulipwa kwa kuzingatia bei ya mnada wa mwezi huo ,mfugaji huyo alitishwa na uongozi wa wilaya kushitakiwa na kulipwa sh.mil.7.
 
Mwanzoni mwa Mwaka huu kampuni hiyo kwa staili hiyo ya kuswaga kwa kutumia magari walizamisha ng’ombe zaidi ya 40 mali ya mkazi wa Motukeri aliyejulikana kwa jina la Kijiji,naye alitishiwa na hakulipwa fidia .
Mwisho,ufuatiliaji unaendelea.

No comments:

Post a Comment