Tuesday, June 18, 2013

BAADA YA NAPE KUITUHUMU CHADEMA, MBOWE NAYE AFUNGUKA NA KUDAI KUWA BOMU LILIRUSHWA NA FFU NA USHAHIDI ANAO


MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe amefichua siri kuhusu tukio la mlipuko wa bomu lililotokea jusi katika viwanja vya Soweto, jijini Arusha.

Katika kauli yake jana, Mbowe ameibua tuhuma nzito dhidi ya Jeshi la Polisi, ambapo alidai kuwa askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) ndiye aliyerusha bomu hilo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa,baada ya kutembelea majeruhi katika Hospitali ya Selian, Mbowe alisema chama chake kina ushahidi wa kutosha juu ya askari huyo kurusha bomu.

Mbowe ambaye pia ni kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni,alisema wamefanikiwa kupata ushahidi wa kutosha juu ya tukio hilo baya linalochafua taswira ya nchi.

Alisema chama chake kipo tayari kuweka ushahidi huo hadharani, iwapo Serikali itaendelea kufanya siasa na kuficha ukweli.


“Tunao ushahidi wa kutosha, ikiwamo wa picha za video unaoonyesha shambulio la bomu na risasi lilivyofanyika katika mkutano wangu jusi eneo la Soweto.

“Picha zinaonesha wazi aina ya silaha zilizotumika kwenye shambulio lile ni tatu, bomu la gurumeti ambalo lilitupwa na askari wa FFU aliyekuwa kwenye uniform.

“Kutokana na ushahidi huu tulikuwa tumewaeleza Polisi kama wataendelea kuficha tutaueleza umma na tutaiambia dunia, kwani aina ya silaha zilizotumika ni SMG na bastola.

“Makasha ya risasi kama ushahidi wa jambo hili zilizotumika tuliyaokota eneo la tukio na tayari tumeyarekodi na kuyakabidhi kwa askari waliokuwa wakichunguza tukio lile,” alisema Mbowe.

Hata hivyo Mbowe alipinga tamko la Serikali kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uratibu na Bunge), William Lukuvi na kusema kauli yake ni ya kitoto mbele ya jamii.

“Kauli ya Serikali kupitia kwa Lukuvi kwamba vurugu zilisababishwa na vikundi, wanasiasa na mashirika yasiyo ya kiserikali ambavyo havijulikani ni sawa na kuwadhihaki Watanzania,” alisema.

Kutokana na hali hiyo Mbowe alisema tayari wanasheria wa chama hicho akiwemo Mabere Marando, Tundu Lissu na Profesa Abdallah Safari wanashughulikia suala hilo.

Alisema baada ya polisi huyo kurusha bomu, alikimbilia katika gari ya Toyota Land Cruizer yenye rangi ya bluu akiongozana na askari mwenzake ambapo gari hilo liliondoka kwa kasi, huku likisindikizwa kwa kukingwa na gari ya TDI hadi kituo cha polisi.


Mtanzania

No comments:

Post a Comment