Sunday, November 25, 2012

Jukwaa la Katiba lamwaga Katiba Mkutano wa Jinsia Morogoro

 Bi Diana Kidala kutoka Jukwaa la Katiba akiwasilisha Mada

                          Wananchi wakifuatilia Mada ya Katiba

Na Mwandishi wa Thehabari.com Morogoro

TAASISI ya Jukwaa la Katiba Tanzania imelazimika kugawa nakala ya Katiba ya Tanzania kwa washiriki wa Mkutano wa Jinsia Ngazi ya Wilaya uliofanyika nje kidogo ya Mkoa wa Morogoro kabla ya kuanza kuelezea umuhimu wa Tanzania kuingia katika mchakato wa kuundwa kwa Katiba Mpya unaoendelea hivi sasa.

Tukio hilo lilitokea juzi Kijijini Mkambarani ulipokuwa ukifanyika Mkutano wa Jinsia ngazi ya Wilaya ulioandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), ambapo Jukwaa la Katiba lilialikwa kutoa mada juu ya umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Katiba mpya.

Idadi kubwa ya wananchi kutoka vijiji mbalimbali walisema hawajawahi iona Katiba hivyo, hivyo Mratibu wa Jukwaa la Katiba, Bi. Diana Kidala kulazimika kutoa nakala ya Katiba kwa wananchi wote kabla ya kuanza mada yake.

Bi. Kidala aliwataka wananchi hao kushiriki kikamilifu katika kutoa maoni juu ya uundwaji Katiba Mpya ili katiba itakayopatikana iweze kuleta mabadiliko kwa kila mwananchi pasipo na ubaguzi wa aina yoyote.

“Tushiriki kwa namna yoyote tutoe maoni yetu ili yaingizwe kwenye Katiba mpya. Katiba ndiyo msingi wa sheria zote...Katiba iliyopo sasa inamapungufu mengi, tunamshukuru Rais Jakaya Kikwete kwa kuona dosari hizo na kuridhia kuanza kwa mchakato wa uundwaji Katiba Mpya,” alisema kiongozi huyo.

Hata hivyo wakichangia wananchi hao katika mkutano huo walioneshwa kushangazwa zoezi la ukusanyaji maoni mkoani kwao (Morogoro) kupita huku wengi wakiwa hawajui chochote wala kushiriki kutoa maoni, jambo ambalo Bi. Kidala alitoa maelekezo kuwa bado wananafasi kushiriki katika zoezi hilo kwa nafasi nyingine.

“Kwa sasa bado mnanafasi ya kutoa maoni kwa kuandika barua kwenye vikundi kwenda Tume ya Katiba, kushiriki katika upendekezaji wawakilishi kwenye mabaraza ya katiba ili wawakilishe maoni yenu, na pia kupendekeza wajumbe na wabunge wa Bunge la Katiba...tuelimishe, tuelimishane na tusichoke kutoa maoni kwani hakuna mtaalamu wala mbumbumbu katika suala hili,” alisema Kidala.

Kwa upande wake TGNP iliwataka wananchi kuunganisha nguvu katika utoaji maoni ili sauti zao ziweze kusikika ipasavyo katika uwasilishaji wa maoni yao kwenye mchakato mzima wa uundaji Katiba mpya.

*Habari hii imeandaliwa na www.thehabari.com

No comments:

Post a Comment