Friday, October 5, 2012

JAMII YAPEWA WITO WA KUWAPENDA WALEMAVU



Wito umetolewa kwa Jamii kuwapenda,kuwaheshimu na kuwathamini watu wenye Ulemavu ikiwemo kuheshimu haki zao na kuwasaidia pale wanapohitaji msaada.


Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Asasi ya Lake Victoria Disability Center (LVDC) Bw. Dennis Maina inayojihusisha na watu wenye ulemavu mkoani Mara.


Amesema Asasi yao imenufaika na ruzuku iliyotolewa na Taasisi ya The Foundation for Civil Society ya jijini Dar es Salaama kwa Mwaka 2011-2012 ambapo asasi hiyo ilipata kiasi cha Shilingi milioni arobaini na nne laki tisa na elfu sitin na sita na mia saba (44,966,700) katika kutekeleza mradi wa Kuwajengea uwezo watu wenye ulemavu na wadau katika mambo ya Ulemavu.


Bw Dennis amesema kuwa toka wameanza kutekeleza mradi huo uliofadhiliwa na Taasisi ya Foundation for Civil Society ya jijini Dar es Salaama kwa Mwaka 2011-2012 wamepata faida kubwa ikiwemo kuwajengea uwezo wa kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu,huku uwelewa katika jamii kuhusiana na mambo ya watu wenye ulemavu kuongezeka na hivyo kutambua haki zao za msingi.


Mbali na hizo lakini pia amesema faida nyingine ni pamoja na Walemavu kuelewa haki zao huku Mahusiano yakionekana kuwa mazuri kati ya Jamii na Watu wenye Ulemavu.Katika kutekeleza mradi huo Bw Dennis amesema kuwa kituo chake kimenufaika na ununuzi wa Vifaa kutokana na ruzuku waliyoipata kutoka Taasisi hiyo pamoja na mradi huo kukamilika.


Ameongeza kuwa faida nyingine ambayo Kituo chake kimepata ni pamoja na kuaminika katika Jamii kutokanma na kujitoa kusaidia Jamii ya watu wenye Ulemavu Mkoani Mara.


Akiongelea mabadiliko yaliyoonekana kutokana na kutekeleza Mradi huo,Mkurugenzi huyo wa LVDC amesema mabadiliko makubwa ni kushamiri kwa mahusiano kati ya watu wenye Ulemavu na wale wasio Walemavu tofauti na ilivyokuwa Mwanzo,watoto wenye Ulemavu kupelekwa Shule huku awali walionekana kutothaminiwa katika masuala ya elimu.


Mabadiliko mengine amesema kuwa ni pamoja na Watu wenye Ulemavu kupewa kipaumbele katika masuala ya Matibabu tofauti na ilivyokuwa  awali huku Semina na Warsha zikionekana kuwasaidia Viongozi katika kutambua haki za watu wenye Ulemavu na Mahitaji yao


Aidha kuhusu kushirikishwa Jamii katika mradi huu ni pamoja na wahuska wa Mradi kuchagua Shule moja kila wilaya mkoani Mara na kufanya nazo kazi hasa lengo likiwa ni kufikisha ujumbe kwa Jamii kuhusu Masuala ya Walemavu.


Mbali na kufanya kazi za kusaidia watu wenye Ulemavu pia Mkurugenzi huyo amesema kuwa waliweza kuendesha Vipindi 45 vya redio (Victoria Fm) ambapo walitumia nafasi hiyo kutoa elimu kuhusiana na Watu wenye Ulemavu huku baadhi ya watu wakipiga simu na kuuliza maswali na kasha kupata ufafanuzi kutoka kwa wataalam wa Masuala ya watu wenye Ulemavu.


Kwa kuelewa ukubwa wa Tatizo la Walemavu katika Jamii Mkurugenzi huyo amesema kuwa asasi yake inaandaa mkakati wa kutanua wigo wa kuzifikia haki za watu wenye Ulemavu katika mkoa wa Mara umeandaliwa ifikapo Desemba 2012.


Bw. Dennis amesema kuwa  kulingana  na Takimu  zilizokusanywa na LVDC mwaka 2010 kwa watu 3600 wenye ulemavu mkoa wa Mara wakati asai hiyo inaendesha mafunzo ya upigaji kura kwa watu wenye ulemavu yaliyokuwa yamefadhiliwa na UNDP na DELLOITE  iligundulika kuwa hakuna mkakati wala mpango kazi  ulioandaliwa na Viongozi wa vyama vya watu wenye Ulemavu .


Katika hatua nyingene Mkurugenzi huyo amesema kuwa asasi yake ina mahusiano chanya na baadhi ya Taasisi hapa nchini na nje ya nchi na ndiyo maana imekuwa ikipata ufadhili katika miradi mbalimbali wanayoiandaa.


Mkurugenzi huyo wa LVDC amesema kuwa pamoja na kuonekana kufanikisha mradi huo vizuri kwa asilimi kubwa lakini bado kumekuwepo na changamoto mbalimbali ambazo zilionekana kuwa kikwazo katika kukamilisha mradi huo ikiwemo pamoja na Jamii kutowathamini watu wenye Ulemavu,asilimia kubwa ya watu wenye ulemavu hawajapata elimu ya awali huku baadhi ya wanajamii wakiendeleza Mila Potofu kwa watu wenye ulemavu katika Familia.


Pamoja na changamoto hizo lakini changamoto zingine ni pamoja na Jamii kutokubali kubadilika katika kuwatambua watu wenye Ulemavu kama watu wengine,kuboresha huduma zinazowahusu watu wenye Ulemavu kutokana na Mazingira yao kutokuwa rafiki.


Bw Dennis Maina alisema kuwa Changamoto zingine ni pamoja na Uwelewa wa watu wenye Ulemavu kuwa mdogo na kuona kile wanachofanyiwa ni sawa huku baadhi ya watu wakiona ni kupoteza muda kumshughulikia mtu mweye Ulemavu na wengine wakiendelea kuwa na mtazamo hasi pamoja na suala la Umaskini katika Jamii pia imeonekana kuwa Changamoto.


Wakiongelea kuhusu faida walizozipata kutokana na mradi huo uliokuwa ukitekelezwa na LVDC kwa ufadhili wa Taasisi ya The Foundation for Civil Society ya jijini Dar es Salaama kwa Mwaka 2011-2012,baadhi ya walengwa wamesema kuwa wamenufaika kwa asilimia kuwa na mradi huo huku wakiomba asasi hiyo kuendelea kuwasaidia hata baada ya Mradi huo kuwa umekamilika.


Kambarage Madaraka mtoto anayesoma darasa la tatu katika Shule ya Msingi Kigera ambaye ana ulemavu wa Miguu amesema kuwa kwa asilimia kuwa amenufaika na mradi huo kutokana na Mafunzo waliyoyapata nay eye kufahamu haki zake kama Mlemavu.
Mbali na Kambarage pia baadhi ya wanafunzi ambao walihusishwa katika Mradi huo wamesema kuwa wamenufaika kwa kupata elimu inayohusiana na Masuala la walemavu lakini wakalaani baadhi ya watu ambao bado wanaendelea kuwatenga watu wenye Ulemavu na kuwanyima haki zao za msingi.


Naye Mwalimu Christina Stephen kutoka Shule ya Msingi Kigera A ambaye hujihusisha na masuala ya Watu wenye Ulemavu shuleni hapo amesema kuwa katika mradi huo amenufaika kutoka na kujua haki za Walemavu,kuwapenda na kuwathamini kama watu wengine.


Katika Shule ya Msingi Nyabange iliyopo wilaya ya Butiama ambapo mradi huu pia umefika umeweza kuwanufaisha zaidi ya Vijana 10 kutoka shuleni hapo huku wengi wao wakisema kuwa wamejifunza mambo mbalimbali yanayohusiana na Masuala ya watu wenye Ulemavu.


Walisema kuwa wamejua haki za Walemavu,kutambua Walemavu,kutowatenga Walemavu,kuwapa haki sawa Walemavu,kuwasaidia Walemavu,kuwapa elimu na Makazi bora watu wenye Ulemavu.


Rajabu Josephat mtoto anayesoma darasa la nne  katika shule hiyo ambaye anaulemavu wa miguu yote miwili amesema kuwa m Taasisi ya The Foundation for Civil Society ya jijini Dar es Salaama kwa Mwaka 2011-2012 umemnufaisha ikiwa pamoja na kusaidiwa baiskeli ambayo imeweza kumrahisishia shughuli zake pamoja na kujua haki zake kama Mlemavu.


Nao Viongozi wa Serikali wakiongelea Mradi huo wamesema kuwa wanaishukuru LVDC na Taasisi ya The Foundation for Civil Society ya jijini Dar es Salaam kwa kufanikisha Mradi huo katika Jamii ya Mkoa wa Mara.


Bw Mfungo Bunini Mtendaji wa Kata ya Mkendo ambapo mradi huo pia umeweza kunufaisha baadhi ya vijana amesema kuwa kujitokeza kwa Taasisi kama The Foundation for Civil Society ni msaada mkubwa kwa Serikali kwani serikali haiwezi kufikia watu wote kwa wakati lakini taasisi kama hizo zinapokuwepo zinasaidia sana katika Jamii


 “Mimi napenda sana kuishukuru hii Taasisi iliyowafadhili hawa jamaa kwani inasaidia Serikali yetu ambayo ina mambo mengi katika Jamii na pia napenda watu wengine wajitokeze kusaidia kama ilivyo taasisi ya The Foundation for Civil Society” alisema Mtendaji huyo


Katika kuufanikisha mradi huo Bw Dennis amesema kuwa ingekuwa kazi ngumu kama wasingeweza kushirikiana na baadhi ya Sekta mkoani Mara kufanikisha zoezi hilo,kwasababu hiyo alisema kuwa wameweza kutoa majalida mbalimbali ambayo yaekuwa yakielezea malengo ya Asasi hiyo na lengo la mradi huo ambapo wanajamii walielewa na kuto ushirikiano.


Mbali na hivyo ameongeza kuwa kumekuwepo na semina za Mara kwa Mara kwa wanajamii zinazohusiana na Masuala ya Walemavu hivyo kwao ilikuwa rahisi kufanikisha mradi huo.


  “Unajua kama tusingeshirikisha jamii inayotuzunguka ingekuwa kazi maana jamii hiyo hiyo bado ilikuwa na Mtazamo tofauti katika mambo yanayohusu Walemavu hivyo tukaona kwanza tuwape vitu ambavyo watakuwa wanasoma ikiwa ni njia ya kuzielewa haki za walemavu lakini pia kuwashirikisha katika Semina mbalimbali tunazoziandaa” alisema Bw Dennis


Akiongelea ufadhili walioupata kutoka The Foundation for Civil Society,Mkurugenzi huyo alisema kuwa wafanyakazi wote wa asasi yake wamekuwa na ufahamu mkubwa kuhusu masuala ya watu wenye ulemavu,kupata uwezo wa kuwahudumia watu wenye Ulemavu tofauti na awali,wameweza pia kujua haki za watu wenye Ulemavu na pia wameweza kupata elimu jinsi ya kutekeleza Mradi kwa ufanisi.


Mbali na kuongelea ufadhili huo,Mkurugenzi huyo ameishukuru Taasisi ya The Foundation for Civil Society kwa ruzuku waliyoipata kwani kwa asilimia kuwa imeweza kusaidia kubadilisha Maisha ya watu wenye Ulemavu kimtazamo na Kimaisha Mkoani Mara.

No comments:

Post a Comment