Saturday, April 6, 2013

Mbunge Mnyika ahaidi kumsomesha mwanafunzi bora Chuo cha Jinsia

 Bendi ya Jeshi la Polisi Tanzania ikiwajibika katika mahafali hayo

 Baadhi ya wafanyakazi wa TGNP wakiwa katika mahafali
 Bendi ya Polisi ikiwajibika
 Maandamano mgeni rasmi na viongozi wa GTI na TGNP
 Maandamano ya mgeni rasmi na viongozi wa GTI na TGNP
 Mgeni rasmi, John Mnyika akizungumza
 Mmoja wa wahitimu wakitunukiwa cheti cha mafunzo ya GTI na mgeni rasmi, John Mnyika

 Mwenyekiti wa Bodi ya GTI,Marry Rusimbi akihutubia

Na Joachim Mushi

MBUNGE wa Jimbo la Ubungo kupitia tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Mnyika ameahidi kumsomesha mwanafunzi bora wa Chuo cha Jinsia (GTI) kupitia sehemu ya mshahara wake wa ubunge.

Mbunge huyo alitoa ahadi hiyo jana jijini Dar es Salaam katika sherehe za Mahafali ya Kwanza ya Chuo cha Jinsia, GTI alipokuwa mgeni rasmi. Alisema anatambua mchango wa chuo hicho katika kuiandaa jamii kupigania usawa wa rasilimali za taifa, hivyo kupitia mshahara wake wa ubunge atatoa mchango wa kumlipia ada mwanafunzi bora wa chuo hicho mwakani.

Mbunge huyo aliupongeza uongozi wa GTI kwa mafanikio waliofikia ya kuanzisha chuo kinachotoa mafunzo ya jinsia kwa jamii na kushauri uongozi kujipanga na kuwasilisha ombi la kuomba fungu la fedha kutoka Mfuko wa Mbunge wa Maendeleo wa Jimbo ili kukiwezesha chuo hicho kufanya shughuli zake kiufanisi.

Awali akizungumza katika mahafali hayo, Mkuu wa Chuo cha GTI, Dk. Diana-Bupe Mwiru alisema mahafali hayo ni ya kihistoria kutokana na kwamba yanafanyika kipindi ambacho Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) ambao ni wamiliki wa chuo hicho wakisherehekea miaka 20 tangu kuanzishwa kwa taasisi hiyo.

"TGNP inasherehekea miaka 20 ya harakati za ukombozi wa mwanamke kimapinduzi dai kuu likiwa rasilimali za nchi kunufaisha watu wote na hasa wale walioko pembezoni. Mwanamke wa kitanzania amekuwa miongoni mwa makundi yaliyoko pembezoni kutokana na mila na sheria kandamizi ambazo zilishindwa kutambua mchango wa mwanamke katika jamii na majukumu makubwa ambayo ameyabeba ili kuhakikisha kuwa jamii inaendelea kuwepo," alisema Dk. Mwiru.

Aliongeza kuwa GTI tangu kuanzishwa kwake imekuwa ikitoa mafunzo kwa umahiri mkubwa katika soko la ndani na nchi za jirani, huku kikiwa kimefundisha washiriki zaidi ya 6000 kutoka nchi za Msumbiji, Nigeria, Malawi, zambia, Kenya, rwanda, Uganda, Ethiopia, Norway pamoja na Tanzania yenyewe.

"Kutokana na umahiri wake katika kutoa mafunzo GTI imeweza kutambuliwa kimataifa kama chuo kilichotukuka katika kutoa maarifa na stadi katika nyanja ya jinsia na maendeleo kwa Afrika Mashariki na Kati. Kwa GTI hii ni hatua ya mafanikio ambayo tuna kila sababu ya kujivunia," alisema Mkuu wa Chuo hicho.

Aidha Dk. Mwiru alitoa shukrani kwa mashirika mfadhili wa GTI ambayo ni 'Foundation for Civil Society, UN Women, UNFPA, Deloitte, Action Aid na SIDA kupitia TGNP na RATN ambayo yamekuwa sehemu ya mafanikio ya chuo hicho. Ikiwa ni pamoja na kuiomba Serikali pamoja na taasisi zake nayo kuanza kukitumia chuo hicho.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Bodi ya GTI, Profesa Saida Othman aliiomba Serikali kushughulikia changamoto ya ubora wa elimu kiujumla kwani matokeo yanavyokuwa mabaya hata vyuo vinavyotegemea wanafunzi hukosa wanafunzi wenye sifa kujiunga na vyuo hivyo.


Jumla ya wahitimu wa 11 walifanikiwa kutunukiwa vyeti vya mafunzo ya jinsia katika mahafali hayo ya kwanza.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com.

No comments:

Post a Comment