Monday, April 22, 2013

Mahakama ya Rufani yashindwa kusikiliza rufaa ya Zombe


Mkuu wa Upelelezi wa zamani wa Mkoa wa Dar es Salaam (RCO), Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Abdallah Zombe.Dar es Salaam,Tanzania
Mahakama ya Rufani Tanzania hivi punde imekwama kusikiliza rufaa ya Mkuu wa Upelelezi wa zamani wa Mkoa wa Dar es Salaam (RCO), Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Abdallah Zombe na wenzake wanane baada ya kubaini kuwapo kwa kasoro kwenye taarifa ya rufaa hiyo.

Kutokana na hali hiyo Jamhuri imeomba iruhusiwe kufanya marekebisho, lakini upande wa utetezi umepinga na kuiomba mahakama hiyo itupilie mbali rufaa hiyo.

Baada ya upande wa utetezi kutoa msimamo huo sasa mahakama hiyo itatoa uamuzi siku nyingine.

Kesi ya Zombe

Zombe na wenzake wanane walikuwa wanakabiliwa na kesi ya mauaji ya wafanyabiashara wa madini ambao wanatoka Tarafa ya Mahenge mkoani Morogoro.

Katika kesi hiyo Zombe na wenzake wanadawa kuwaua Sabinus Chigumbi, maarufu kama Jongo na ndugu yake Ephrahim Chigumbi, Mathias Lunko, Mbena dereva teksi Juma Ndugu katika msitu wa Pande uliopo Mbezi Luis, Jijini Dar es Salaam.

Mauaji hayo yalifanyika Januari 14, mwaka 2006 na awali baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es  Salaam kusikiliza ushahidi wa pande zote Agosti 17, 2009, mahakama hiyo ilisema  upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yao.

Awali Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) alikata rufaa Mahakama ya Rufani, kupinga hukumu ya Mahakama Kuu, akidai Jaji Salum Massati alikosea kuwaachia huru washtakiwa hao, akidai kulikuwa na ushahidi wa kutosha kuwatia hatiani.

Rufaa hivyo imesikilizwa na Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani. Jopo la majaji hao limeongozwa na Jaji Edward Rutakangwa, akisaidiana na Jaji Bernard Luanda na Jaji Salum Mbarouk.

Katika rufaa hiyo namba 254/2009, iliyofunguliwa mahakamani hapo Oktoba 6, 2009.

No comments:

Post a Comment