Na Mwandishi wa Thehabari Korogwe Vijijini
BAADHI ya walimu na wazazi wa Halmashauri ya
Wilaya ya Korogwe wameiomba Serikali kutenga bajeti maalumu kwa ajili ya
kuboresha elimu ya awali ili madarasa hayo yasiwe mzigo kwa walimu wakuu.
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari
hizi eneo hilo umebaini licha ya Serikali kusisitiza kila shule ya msingi kuwa
na darasa la awali, baadhi ya maeneo haitoi fungu lolote kuendesha madarasa
hayo.
Akizungumza hivi karibuni ofisini kwake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya
Msingi Kwagunda, David Kituja iliyopo Kijiji cha Kwagunda Korogwe, alisema darasa la awali shuleni hapo hutumia
bajeti ile ile ya shule ya msingi, jambo ambalo limekuwa mzigo kwa walimu wakuu
hivyo kushauri kuongeza fungu kuboresha darasa hilo.
“Madarasa ya awali kweli ni tatizo, maana
inasikitisha Serikali inasisitiza yaanzishwe kwa kila shule lakini hakuna
bajeti yoyote iliyotengwa kuyahudumia...mwalimu unalazimika kubana upande wa
bajeti ya msingi uitumie kwenye darasa la awali sasa hii ni changamoto kweli kweli,”
alisema Kituja.
Kwa upande wake, mmoja wa wazazi, Vedastus
Mhilu alisema, changamoto ya kipato kwa wazazi wengi vijijini bado ni tatizo
kubwa kwa uchangiaji wa madarasa hayo jambo ambalo husababisha elimu hiyo
kuendeshwa kwa kubabaisha.
“...Huku wazazi wengi ni wakulima kwa hiyo ile
fedha tunayoipata haitoshelezi kuwapeleka watoto wetu kusoma madarasa ya awali au
kuchangia ada na hata michango ya chakula, si kwamba hatupendi watoto wetu wapitie
elimu hiyo ya awali tatizo ni kipato,” alisema Mhilu.
Aidha Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi
Kwashemshi, Jonathan Mzava alisema kwa upande wao wameweza kuanzisha madarasa
ya awali kwa ushirikiano na Serikali lakini kikwazo ni namna ya kupata walimu
wa kudumu kuwafundisha watoto hao muda wote.
“Hapa shuleni ninao wanafunzi kama 100 hivi wa
elimu ya awali, madarasa haya yanaendeshwa kwa msaada wa Serikali ila mwakani
nafikiria kuwashirikisha wazazi ili tuweze kuiboresha zaidi...nitawaomba
wachangie kiasi kidogo ili tuweze kupata walimu ambao muda wote watakuwa wanawafundisha
watoto tofauti na sasa ambapo natumia walimu wa shule ya msingi,” alisema
Mzava.
Akizungumzia kuhusu elimu ya awali, Kaimu Ofisa
Elimu Sekondari, Shaban Shemzighwa alisema hakuna walimu wanaoajiriwa maalumu
kama walimu wa madarasa ya awali hadi sasa, hivyo shule zenyewe hujitegemea
kimgawanyo wa walimu kuendesha elimu hiyo.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com kwa kushirikiana na HakiElimu
No comments:
Post a Comment