Monday, November 5, 2012

Jinsi elimu duni inavyohatarisha amani – Madaraka Nyerere

Nimewahi kuuliza waandishi wa habari wawili, mmoja toka Kenya na mwingine Mtanzania, swali moja: raia wanaamini yuko kiongozi ambaye si mwizi? Mkenya alisema Wakenya wote wanaamini kuwa viongozi wao siyo waaminifu. Mtanzania naye alisema Watanzania wengi zaidi nao wanaamini kuwa viongozi wetu siyo waaminifu.
 
Madhumuni ya msingi ya kutoa elimu ni kumwezesha mwanafunzi kusoma, kuhesabu, na kuandika. Madhumuni mengine ya muhimu ni kumwezesha mwanafunzi kuwa mdadisi, mchambuzi, mwenye uwezo wa kufikiri, na hata mwenye uwezo ya kupinga kwa hoja yale ambayo anafundishwa. Pengine hili la pili lingeweza kuwa muhimu kuliko lile la kwanza kama isingekuwa haiwezekani kupata uwezo huu wa pili bila kuwa na uwezo wa kusoma, kuhesabu, na kuandika.

Hali duni ya elimu iliyopo sasa inatoa nafasi ndogo sana kwa wanafunzi kuvuka ngazi ya kwanza na kuingia ngazi ya pili. Tunao wanafunzi wa sekondari wasiokuwa na uwezo wa kusoma na kuandika. Tunao wahitimu wa elimu ya juu ambao hawana uwezo wa kuridhisha kulinganisha na wenzao waliosoma miaka ya sitini na ya sabini.

Maisha ya baadaye ya hawa watoto yatakosa amani iwapo mfumo wa elimu hautaboreshwa.Leo hii wanaopta elimu nzuri ni asilimia ndogo sana ya mamilioni ya Watanzania ambao wanapata elimu hafifu. Kwa sababu hii kila mwaka ongeko la Watanzania wenye uwezo wa kuchambua, kutafakari, kudadisi, na kupinga kwa hoja masuala mbabali mbali wanazidi kupunguka na tena kwa kasi kubwa.

Siasa ya vyama vingi imefanikiwa kifuchua maovu mengi ya siasa za chama kimoja, lakini pia vyama vingi vimejenga pia imani kwa mwananchi wa kawaida kuwa kila mtu ni mwizi. Juzu juzi nimetoka kupanda Mlima Kilimanjaro na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Loreto na nilimsikia mmoja wao akisema kuwa “kila mtu ni mwizi.”

Hatuwezi kuacha kulaumu mienendo ya baadhi ya viongozi wetu ambayo inawafanya raia waamini kuwa viongozi wa umma waaminifu hawapo tena.

Elimu hafifu inapunguza uwezo wa raia wa kuchambua masuala mbali mbali, lakini siasa ya vyama vingi imefanya kazi nzuri ya kumfanya raia ashuku kila kitu na kila mtu. Kwa taratibu za kisheria za mfumo wa sheria unaojulikana kama civil law ni wajibu wa yule anayetuhumiwa kuthibitisha kuwa siyo mwizi, au hafanyi janja janja ya aina fulani anapokuwa kiongozi au mtumishi wa umma.

Hatari ya hali hii ni kuwa hata pale jambo linapokuwa halina mizengwe ni vigumu kwa raia kuamini hivyo. Raia wanapokuwa hawana tena imani na viongozi na mfumo wa utawala, misingi ya amani itaanza kupata nyufa. Na matukio ya miaka ya hivi karibuni yanaashiria kuwa miaka ijayo haitakuwa na amani ambayo Watanzania wamekuwa nayo kwa muda mrefu.

Madaraka via Muhunda blog

No comments:

Post a Comment