Wednesday, September 12, 2012

HABARI KUTOKA MKOANI ARUSHA

Taasisi ya Trade Mark East Africa (TMEA) imezindua mfuko wa thamani ya dola za Kimarekani milioni 7.5 kufadhili miradi ya ubunifu katika nchi tano wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) inayolenga kuondoa vikwazo vya biashara katika kanda hiyo.
TMEA ni taasisi inayofadhiliwa na mashirika mbalimbali ili kuunga mkono juhudi za kusukuma mbele masuala ya mtangamano hususan ni katika biashara na uchumi katika kuimarisha mkataba wa mtangamano wa EAC.
Mradi huo unaojulikana kama ‘’Mfuko wa Changamoto wa Taasisi ya Trade Mark East Africa ‘’ uliziduliwa rasmi katikati  mjini Kigali, Rwanda na Mkurugenzi wa Afrika Mashariki wa taasisi hiyo, Mark Priestly.
Mfuko huo utakaoendeshwa kwa kipindi cha miaka mitatu unalenga sekta binafsi na vyama vya kiraia, Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki (EANA) limeripoti.
 Priestly alibainisha kuwa changamoto kama vile kuwepo kwa vikwazo visivyo vya ushuru na mchanganyiko wa vuzuizi vya usambazaji, ni masuala ambayo bado yanazuia mtiririko mzuri wa uendeshaji wa biashara katika kanda.
“Sisi hasa tunatafuta ubunifu na mawazo mapya ya kuchangamsha biashara katika Jumuiya EAC na kukabiliana na changamoto ambazo inakumbana nazo,” aliongezea.
Uwekezaji mkubwa katika ubunifu wa miradi ulianza na sekta binafsi na vyama vya kiraia ambavyo vinaweza kukuza biashara katika kanda ndani ya EAC.
Mfuko huo umeshaanzishwa nchini Kenya na Tanzania na muda si mrefu utazinduliwa pia katika nchi za Burundi na Uganda.
Waziri wa Viwanda na Biashara wa Rwanda, Francois Kanimba, alisema mfuko huo ni mpango mwafaka ambao utakuza juhudi za nchi yake kubadilisha uchumi na kuwa mhimili wa kutoa huduma kupitia usafirishaji bidhaa kwa wingi nje ya nchi.
Alisema Mfuko huo unatoa nafasi kwa Wanyarwanda kushindana kikanda kwa kuutumia ili kuendeleza biashara zao.
Na Nchi wananchama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) zitaendelea kufanya mashauriano zaidi juu ya maombi ya nchi mbili za Sudani Kusini na Somalia kutaka kujiunga na jumuiya hiyo yenye wanachama watano.
Uamuzi huo ulifikiwa mwishoni mwa mkutano wa Baraza la Mawaziri la EAC, ambalo ni chombo cha Sera cha Jumuiya hiyo, mjini Bujumbura nchini Burundi.
Vyanzo kadhaa kutoka katika mkutano huo vililiambia Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki (EANA) kuwa Baraza lilikuwa na maoni kwamba maombi ya nchi hizo mbili ambayo yaliwasilishwa mwaka jana na mapema mwaka huu yanahitaji muda zaidi ili yaweze kufikiriwa na jumuiya hiyo ya nchi za Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda na Burundi.
“Baadhi ya nchi wanachama zinahitaji muda zaidi kujadiliana na wadau wote kuhusu taarifa za kamati za uhakiki juu ya maombi ya Sudani Kusini,” vyanzo hivyo vimesema.
Ilikubaliwa kuwa taarifa ya timu ya wahakiki iliyotumwa Juba mwezi Julai kutathmini matayarisho ya Sudani Kusini kujiunga na EAC itawasilishwa katika kikao kijacho cha Baraza la Mawaziri mjini Nairobi,Kenya, Novemba mwaka huu.
Kuhusu maombi ya Somalia, mawaziri hao walibainisha kuwa jambo hilo linahitaji majadiliano ya ziada na wadau zaidi wa kimataifa wanaojihusisha na juhudi za kuleta amani nchini Somalia.
Hata hivyo, Baraza lilimwelekeza Katibu Mkuu wa EAC kuwasilisha maombi ya Mogadishu katika kikao kijacho cha wakuu wa nchi wanachama.

No comments:

Post a Comment