MARA YAANZISHA DOLIA YA WAVUVI HARAMU ZIWA VICTORIA
Na Shomari Binda
Musoma,
Kufuatia kuongezeka kwa uvuvi haramu katika ziwa victoria
kitengo cha udhibiti uvuvi haramu kanda ya Mara kimeanzisha doria
maalumu ya kupambana na watu wanaojihusisha na uvuvi haramu na
uuzaji wa nyavu na makokoro ya kuvulia samaki katika ziwa
Victoria.
Akiongea na waandishi wa habari baada ya
kuanza misako kadhaa na kufanikiwa kuwakamata watu wanaojihusisha
na uvuvi haramu wakiwa nasamaki wadogo tani 3 na nyavu haramu
zinazotumika kuvulia samaki wadogo afisa mfawidhi mdhibiti na
doria kanda ya Mara bwana Braison Meela alisema kikosi cha
udhibititi kitaendelea na msako huo kwa muda wote.
Alisema
msako huo utaendelea katika maeneo mbalimbali ikiwemo maduka ya
wafanyabiashara wanaouza nyavu ili kuona mianya inayoingiza nyavu
haramu katika mkoa wa Mara.
Braison alisema licha ya
Serikali kupiga marufu kwa vitendo hivyo bado kuna watu wasio waaminifu
amao wanaendeleza shughuli za uvuvi haramu kwa kutumia nyavu
zisizoruhusiwa.
Alisema ili kufanikisha zoezi hilo aliwaomba
wananchi wema kuendelea kutoa taarifa katika kikosi hicho ili
kusaidia kupatika kwa watu wanaojihusisha na uvuvi haramu ili
waweze kushughulikiwa kwa mujibu wa sheria kwani wamekuwa
wakisababisha upotevu wa raslimali za Taifa.
Kwa upande
wake Afisa Oparesheni doria na uvuvi kanda ya Ziwa Ally mzee said
alisema oparesheni hizo zitakuwa endelevu kwani kikosi
kimejipanga kuihakikisha kina komesha uvuvi haramu mkoani Mara.
Alisema wale wote wanaojishughulisha na masuala ya uvivi haramu waache
mara moja na kusalimisha bidhaa wanazozitumia ili kujiepusha na matatizo
ambayo watayapata kutokana na Serikali kujipanga vizuri kuhakikisha
inakomesha shughuli hizo na kuwafikisha Mahakamani wale wote
watakaopatikana na hatia.
Kikosi cha doria na
udhibiti wa uvuvi haramu mkoani Mara ni moja ya vikosi
vilivyopo katika mikoa minne iliyopo katika ziwa Victoria
vinavyopambana na shughuli za uvuvi haramu.
Kikosi hicho awali
kimekuwa kikikabiliwa na ukata wa vitendea kazi kwa ajili ya
kupambana na uvuvi haramu ikiwa ni pamoja na magari mafuta na
fedha kwa ajili ya shughuli hiyo hali inayosababisha zoezi
hilo kuwa gumu.
No comments:
Post a Comment