Friday, September 14, 2012

MKUU WA WILAYA YA HANDENI AWATAKA VIJANA KUANZISHA MASHAMBA YA MITI YA MATUNDA ILI KUJIKOMBOA KIUCHUMI

Na Mohammed Mhina, Handeni
HANDENI IJUMAA SEPTEMBA 14, 2012. Mkuu wa wilaya ya Handeni Mkoani Tanga, Bw. Muhingo Rweyemamu, amewataka vijana wanaojishughulisha na biashara ndogo ndogo zikiwemo za matunda, kujiunga katika vikundi na kuanzisha mashamba ya miti ya matunda badala ya kuwa wakaakati.
Mkuu huyo wa Wilaya ametoa wito huo wakati akizungumza na Vijana katika maeneo ya Chanika na Segera mpakani mwa wilaya za Handeni, Korogwe na Muheza mkoani Tanga.
Bw, Rweyemamu amesema kama vijana watajiunga katika vikundi na kuanzisha mashamba ya miti ya matunda wataweza kunufaika kwa kuinua vipato vyao na kubadilika kimaisha.
Amesema kazi ya uchuuzi wa matunda kwa kuyatembeza mikononi, hayataweza kuwakomboa kiuchumi kwa vile faida kubwa itaishia kwa wakulima wanakochukua matunda hayo tofauti na kama watakuwa na mashamba yao.
Hata hivyo, Mkuu huyo wa wilaya ya Handeni amesema kama vijana wataungana na kuanzisha vikundi vya ushirika itakuwa rahisi kwa Serikali kuwapatia huduma zikiwemo za mikopo ya kukuza mitaji yao.
Amesema tayari wilaya ya Handeni imenunua matrekta kwa ajili ya kuwalimia watu mbalimbali wakiwemo vijana wenye vikundi vya ushirika.
Mkuu huyo wa wilaya ya Handeni amewataka vijana hao kuiga mfano wa vijana wenzao wa Kijiji cha Misima wilayani humo ambao wamejiunga pamoja na kuomba kupatiwa eneo la Kilimo kutoka Serikali ya Kijiji.
Katika ziara hiyo, Bw. Rweyemamu alifuatana na wataalam mbalimbali wakiwemo Maafisa Ushirika wa wilaya hiyo ambao nao wamekuwa wakitoa elimu za masuala ya ushirika.
Idadi kubwa ya Vijana waliopo katika Wilaya ya Hendeni, wamekuwa wakijishughulisha na masuala ya biashara ndogondogo zikiwemo za matunda mbali ya kuwepo kwa maeneo makubwa ya kilimo.

No comments:

Post a Comment